Thursday, February 16, 2017

REA kutoa mafunzo ya Nishati

NA FELISTA HENRY

WAKALA wa Nishati Vijijini (REA) wanatarajia kutoa mafunzo ya majuma mawili kwa mafundi na waendelezaji wa vyanzo vya umeme unaozalishwa kutokana na rasimali za nishati jadidifu.
Serikali kupitia REA imeanza utekelezaji wa mradi kabambe wa awamu ya tatu wa kusambaza nishati vijijini utakaojumuisha vijiji 7,873 katika wilaya na mikoa yote ya Tanzania Bara ambao utatekelezwa kuanzia mwaka huu wa fedha hadi 2020/21.
Mkurugenzi Mkuu wa Nishati vijijini Mhandisi Boniface Gissima amesema malengo ya mafunzo hayo ambayo yataanza mwishoni mwa Aprili  hadi Juni mwaka huu ni kuwajengea uwezo mafundi na waendelezaji wa teknolojia waliopo maeneo ya vijijini ili waweze kutoa huduma bora na endelevu.
Mikoa itakayohusika na mafunzo hayo ni Mara, Geita, Tabora, Simiyu na Arusha ambako mafunzo kuhusu nishati itokanayo na mionzi ya jua na utayarishaji wa mpango biashara yatatolewa.
Hata hivyo Gissima amewataka waombaji wa mafunzo hayo wawe na elimu ya kidato cha nne huku wenye vyeti vya ufundi VETA  daraja la kwanza watapewa kipaumbele na watume kabla ya Machi 17 mwaka huu.

0 Comments:

Post a Comment