Monday, August 18, 2025

Lawama Makatibu Kata CCM Hai Kura za Maoni

HAI, KILIMANJARO

Baada ya Kura za Maoni za Chama cha Mapinduzi  (CCM) wilayani Hai mkoani Kilimanjaro kufanyika mengi yameibuka baada ya baadhi ta majina ya wagombea kushindwa kupenya katika ngazi ya udiwani huku kidole cha lawamani kikielekezwa katika ngazi ya chama kwa kile kinachodaiwa kuwabeba baadhi ya wagombea katika kura za maoni.

Baadhi ya wanachama wa CCM wilayani humo (majina yao yamehifadhiwa) wamekiri kuwa mchakato wa kura za maoni uliofanyika hivi karibuni katika wilaya ya Hai haukwenda  kama ilivyotarajiwa  kutokana na dosari mbalimbali kujitokeza.

Wanachama hao wanadai kuwa wakurugenzi wa uchaguzi walikuwa wakionyesha hisia zao kwa mgombea  badala ya kuwa wasimamizi wa zoezi zima la kura za maoni.

“Kwa mujibu wa muundo wa chama, makatibu wa kata  ndio watendaji  na kwa nyakati za uchaguzi hugeuka kuwa wasimamizi wa haki na taratibu. Lakini katika uchaguzi huu makatibu wa kata waliweka kando dhamana hiyo na kuwa wapambe wa mgombea ubunge Saashisha Mafuwe,” alisema mwanachama wa CCM.

Aidha baadhi ya wanachama hao wa CCM walidai kuwa siku ya kura za maoni wajumbe walihusika waziwazi  kupokea kiasi cha shilling 50,000; pia wengine walisafirishwa na magari kuelekea katika mkutano wa kura za maoni na baadhi ya wagombea wa udiwani na ubunge.

“Wajumbe wa kamati ya siasa na wasimamizi waliotumwa katika kata ikiwamo kata ya Bondeni alionekana wazi kuendesha kampeni na kutoa maelekezo kwa wajumbe kumpigia kura mgombea Saashisha Mafue,” alisema mwanachama huyo wa CCM.

Wanachama hao wanadai kuwa kutokana na dosari hizo ni wazi kwamba zimeshusha hadhi ya chama chao kwa watanzania  hatua ambayo inaweza kuwa na athari katika kupeleka maendeleo kwa jamii inayowazunguka.

“Hebu fikiria katika kazta zote wajumbe wasio halali  waliingizwa kwa maelekezo ya makatibu kata. Baadhi ya nafasi za wajumbe  waliokufa  zilijazwa bila kufuata utaratibu na baadhi ya wajumbe walipiga kura mara mbili, inaleta picha gani kwa jamii?” alisema mwanachama wa CCM.

Akizungumza kwa njia ya simu Katibu wa CCM wilaya ya Hai Hamis Mkaruka Kura alikiri kumsimamisha  Katibu Kata wa Machame Kaskazini baada ya kukiuka utaratibu baada ya kuandika barua makanisani na misikitini kuhimiza waumini wamchague Saashisha Mafuwe.

“Uchaguzi ulienda vizuri tu; sasa wanapodai kuwa makatibu kata waliharibu kura za maoni kwa kuwa wapiga kampeni  sio kweli; wanatokana katika vyumba vya kupigia kura wakati wao ni wasimamizi, mengine ni hearsay,” alisema Katibu huyo.

Katibu huyo aliongeza kusema tuhuma za rushwa ni mambo ya kusikia kwani hadi sasa hajaletewa ripoti yoyote ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuhusu vitendo vya rushwa wakati wa kura za maoni wilaya ya Hai zilipofanyika.

Mgombea ubunge wa Jimbo hilo Saashisha Mafuwe ambaye yupo katika kinyang’anyiro ndani ya chama katika nafasi hiyo alipotafutwa kuzungumzia sakata hilo alikata kuzungumza akisema mambo yote chama ndicho kinasimamia.

“Kwa sasa siwezi kusema lolote; kama unataka kuhusu hayo kawaone chama watakueleza mimi kwa  sasa hapana,” alisema Mafuwe.

Kwa upande wake Mkuu wa Takukuru mkoa wa Kilimanjaro Mussa Chaulo alisema hadi sasa hajapokea taarifa yoyote ya vitendo vya rushwa kutoka wilaya ya Hai kwani yupo nje ya ofisi kwa majuma mawili.


0 Comments:

Post a Comment