Ukweli na Kuheshimiana ni kiini ujenzi wa jamii zetu

Ulimwenguni kwa sasa kumejaa habari potofu na upotoshaji, ni muhimu kuhakikisha kwamba ukweli na kuheshimiana vinakuwa kiini kwa ujenzi wa jamii zetu.

Mapambano dhidi ya Habari za Uongo hayapaswi kukoma

Habari za uongo, habari za uongo zinazosambazwa kwa lengo la kumdhuru mtu au jambo fulani, huifanya jamii kuwa na sintofahamu. Zinaweza kutumika kwa madhumuni ya kiitikadi, kisiasa au hata uhalifu, kama vile ulaghai mtandaoni unaolenga kuiba data ya kibinafsi.

Utandawazi na Athari zake katika Uandishi wa Habari

Katika jamii yetu ya kisasa, ambapo habari ziko kila mahali na zinaweza kupatikana kwa kila mtu, mara nyingi ni ngumu kutofautisha kati ya vyanzo vya kuaminika na habari bandia.

Uandishi wa Habari nguzo msingi mkuu kwa ujenzi wa jamii inayojitambua

JAIZMELA blog ni miongoni mwa vyanzo vya habari, zilizochakatwa kwa kuzingatia miiko ya uandishi wa habari.

Mila na Desturi ni nguzo muhimu

Mila na desturi ni nguzo muhimu sana katika utamaduni wa jamii yoyote ile; mila ni sawa na sheria zisizoandikwa. Mila ni taratibu za maisha na mwenendo zinazofuatwa na jamii fulani katika utendaji kulingana na historia na utamaduni wao. Mila zinatambulisha maadili ya jamii husika, huelezea namna jamii inavyoendesha mambo yake.

Tuesday, June 3, 2025

Sakata la Askofu Gwajima

 

Jeshi la Polisi limezua gumzo usiku wa kuamkia leo baada ya kulizingira Kanisa la Ufufuo na Uzima, linaloongozwa na Askofu Josephat Gwajima, wakati wa ibada ya maombi ya usiku maarufu kama mkesha.


Tukio hilo lililotokea majira ya saa nne za usiku, wa tarehe 2 Juni 2025 katika eneo la Ubungo jijini Dar es Salaam lilipo kanisa hilo ambapo hatua hiyo imeibua maswali mengi miongoni mwa waumini na watanzania kwa ujumla kuhusu dhamira na ujumbe ulioambatana na hatua hiyo ya vyombo vya dola.


Kulishuhudiwa polisi wakiwasili kwa magari kadhaa na kuimarisha ulinzi nje ya majengo ya kanisa hilo, hatua ambayo iliwafanya waumini wengine kusalia ndani na wengine nje ya kanisa hilo.


Hayo yanajiri kukiwa na taarifa za kanisa lake kufungiwa kuendesha ibada zake na mamlaka za serikali jambo ambalo amelikanusa mapema leo tarehe 3 Juni 2025.


Kwa upande wa waumini na wanaharakati wa haki za binadamu, hatua hiyo inaweza kutafsiriwa kama kuingilia uhuru wa kuabudu, jambo ambalo linaweza kuleta taswira hasi kwa serikali katika macho ya umma na kimataifa. Katika tukio hilo kuamkia la usiku kulisikika waumini wakisema uhuru wao wa kuabudu unazuiwa huku wakirusha mawe kuwaondoa askari hao.


Kwa kuwa Askofu Gwajima ni kiongozi wa dini na pia mbunge wa Kawe kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi ambaye kwa sasa ameshikilia msimamo wa kusema ukweli kuhusu vikundi vya watekaji, tukio hilo linaingiza mchanganyiko wa dini, siasa, na usalama.

Hii inatoa taswira ya hali tete ambapo mipaka kati ya mihimili hiyo mitatu inaanza kuchanganyika. Mchungaji Dickson Kabugumila amekaririwa akisisitiiza hali ambayo itatokea ndani ya Chama cha Mapinduzi mwaka huu.


Kufuatia tukio la Polisi kuzingira Kanisa la Ufufuo na Uzima; Rais wa Chama cha Wanasheria nchini Tanganyika Law Society Boniface Anyisile Mwabukusi ameweka bayana kuwa kwa sasa hawatakiwi tena kujifanya hawamjui anayewateka watu hapa nchini.

Wakili Mwabukusi ameandika katika ukurasa wa Facebook, maneno haya “Mtekaji amepata ujasiri yuko tayari kufanya chochote hadharani kuzuia tusipige kelele za Utekaji. Sisi tunaotekwa na kupotelewa na ndugu tuendelee kumuonea Aibu na upuuzi wake huu? La hasha ......Kanisa Linashambuliwa, kwa Kusimama katika Kweli. Tukatae dhuluma hii.Tuna haki ya kujilinda...tuna haki ya kulinda ndugu zetu na rafiki zetu....Usikae kimya tena"

Awali Askofu Gwajima alithibitisha kuhusu Askari wa Jeshi la Polisi kuzingira kanisa lake wakati wa usiku wakiendelea na huduma  Kanisa hapo.


Baadhi wa wafuatiliaji wa masuala ya siasa za ndani na nje ya Tanzania wanasema Katika mazingira ya sasa, sauti za viongozi wa CCM kuhusu masuala nyeti zimesikika kwa nadra sana au hazipo kabisa. Badala yake, sauti za kejeli, vitisho, au ukosoaji wa upinzani ndizo zinazopewa kipaumbele ikiwa ni ishara ya chama kilichojikita zaidi katika kujilinda kuliko kuwatumikia wananchi.


Hata hivyo Katibu wa zamani wa Itikadi,Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) aliwahi kutoa tahadhari kuhusu uwepo wa serikali za kihuni ndani ya mamlaka kamili katika chama au serikali iliyopo madarakani.


Kwa upande wake mwanaharakati na mwandishi wa habari mwandamizi Cyprian Musiba aliwahi kukaririwa akikitahadharisha Chama cha Mapinduzi kuhusu mabadiliko ya dunia ambayo kwa sasa kuna serikali za kihuni dunia ambazo zinataka vyama vyote vilivyokaa madarakani kwa muda mrefu kuondolewa.


Wakati Chama Cha Mapinduzi (CCM) kikiwa bado kina mtandao mpana wa kisiasa na miundombinu ya uongozi nchini, ukimya wake katika masuala nyeti unatoa ishara hatari: kwamba chama hicho huenda hakina tena msukumo wa kisiasa wa awali wa kutetea wanyonge, bali kimegeuka kuwa sehemu ya mfumo unaotajwa kuwa wa kukandamiza sauti mbadala. Wananchi wanaanza kuhoji — si tu kwa kelele mitandaoni, bali kwa ukimya wa kutojihusisha, kuonyesha kukata tamaa, au kutafuta mabadiliko nje ya mfumo rasmi wa kisiasa.

Monday, May 19, 2025

KESI YA TUNDU LISSU: Bashasha, Nderemo, Vifijo vyatawala Mahakama ya Kisutu

 

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Tundu Lissu muda mchache kabla ya kesi kuanza mnamo tarehe 19 Mei 2025 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini  Dar es Salaam. (Picha na; MTANDAO)

Bashasha, nderemo, na vifijo vimedhihirika kwa maelfu ya wafuatiliaji wa siasa za ndani katika Tanzania baada ya kumuona Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Tundu Lissu wakati akipandishwa kizimbani kwa ajili ya kuendelea na kesi inayomkabili ya Uhaini.

Shangwe hizo zinaashiria mgawanyiko mkubwa wa kisiasa nchini, ambapo siasa imegeuka kuwa jambo la hisia kali, na si la hoja. Badala ya kuangalia uzito wa tuhuma na mchakato wa haki, baadhi ya watu wanaona haya ni mafanikio ya kisiasa dhidi ya wapinzani wao.

Tundu Lissu alipandishwa kizimbani leo tarehe 19 Mei 2025 akitokea mahabusu anakoshikiliwa na vyombo vya usalama kutokana na mashtaka yanayomkabili, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Tofauti na wakati wa kwanza leo katika viunga vya mahakama hakukuwa na purukushani yoyote ya Jeshi la Polisi hatua ambayo imedhihirisha kuwa Kama polisi wangekuwepo kwa wingi, hali hiyo ingeweza kufasiriwa kama vitisho, hasa kwa wananchi waliokusanyika kwa amani na badala yake kunatoa nafasi ya hali ya utulivu na ya ki-demokrasia kushamiri nchini.

Katika ukumbi wa mahakama Lissu alionekana kuzungumza maneno mazito kuhusu mustakabali wa kesi hiyo hali akiendelea kusisitiza kuhusu msimamo wa chama chake wa “No Reforms, No Election”.

Aidha baada ya kuendelea na mashtaka hayo Makamu Mwenyekiti wa Chadema Joh Heche alipokelewa na mamia ya wafuasi wa chama hiyo.

Heche alisisitiza kuwa Lissu atarudi tena mahakamani hapo mnamo tarehe pili ya Juni 2025 kuendelea na mashtaka hayo huku akisisitiza baada ya kikao cha kamati ya utendaji wataendelea na mikutano ya “No Reforms, No Election”.

Shangwe za wafuasi wa siasa dhidi ya mtu anayekabiliwa na mashtaka mazito kama uhaini hazipaswi kuchukuliwa kuwa ni jambo la kawaida au la kusherehekea. Badala yake, zinahitaji tafakari ya kina kuhusu mwenendo wa siasa, hali ya demokrasia, na maadili ya taifa. Ni muhimu jamii itofautishe kati ya ushindani wa kisiasa na kuunga mkono misingi ya haki, utu, na demokrasia.

Sunday, May 18, 2025

Papa Leo XIV achagua kuishi Vatican Apostolic Palace, aikacha Santa Marta Motel

Baada ya kuchaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki duniani Papa Leo XIV ameanza rasmi kuishi katika nyumba ya kipapa iliyopo Vatican.

Wengi walikuwa na maswali kuhusu suala hilo kama atafuata nyayo za mtangulizi wake Papa Francis aliyekuwa akiishi pasipo anasa katika Nyumba za Wageni za Vatican.

Papa Francis aliweka rekodi ya kuwa papa wa kwanza kukataa kuishi katika Kasri la Vatican baada ya miaka 143 ambapo alichagua kuishi Santa Marta Motel, Vatican.

Papa Leo XIV amechagua kuishi katika Kasri la Kitume la Vatican (Vatican Apostilic Palace) kwa ajili ya kuendelea na huduma yake kulisimamia Kanisa Katoliki duniani.

Vatican Apostolic Palace ni jengo ambalo lilisanifiwa na kuanza kujenga mnamo karne ya 15 kwa usanifu wake Donato Bramante katika muundo wa Reinaissance.

Kipindi  hiki cha Renaissance kilikuwa cha mabadiliko makubwa ya kisanaa, kielimu, na kifalsafa kilichoanzia katika ardhi ya Italia kwenye karne ya 14 na kuenea Ulaya nzima hadi karne ya 17.

Katika sanaa ya majengo, kipindi hiki kilihama kutoka kwa usanii wa kati wa kighorofa yaani Gothic na kuzingatia upya kanuni za uzuri, usawa, na mantiki zilizoasisiwa na Warumi na Wagiriki wa kale.

Moja ya majina makubwa katika kipindi hiki ni msanifu wa jengo la sasa la Vatican Apostolic Palace; Donato Bramante, ambaye alichangia sana kuasisi na kuendeleza staili ya usanifu ya Renaissance ya juu.

Vatican Apostolic Palace imeundwa na vyumba 1000 ikiwamo sehemu ya kukaa, kulala na kliniki ya dawa. Jengo hili pia lina Kanisa la Sistina ambalo ni mojawapo ya majengo mashuhuri zaidi duniani, hasa kutokana na uzuri wa sanaa yake ya ndani, hasa michoro ya dari  inayoonyesha Hukumu ya Mwisho iliyochorwa na Michelangelo.

Papa Leo XIV anajitokeza kama kiongozi mwenye maono makubwa ya kurejesha Kanisa katika misingi yake ya asili: kiroho safi, maadili mema, na uaminifu wa ndani kwa injili ya Kristo.

Dunia ya sasa inakabiliwa na changamoto nyingi, kuanzia mmomonyoko wa maadili, maisha ya kiroho kupoa, hadi migogoro ya ndani ya taasisi ya Kanisa.

Hali hii inamtia moyo Papa Leo XIV kuchukua hatua madhubuti za kufufua maisha ya kiroho na kimaadili miongoni mwa waumini, pamoja na kufanya mageuzi ya ndani ya Kanisa yanayolenga uwazi, usafi wa utume, na kujibu hitaji la kizazi cha sasa.

Tukirejea kwake; Donato Bramante alizaliwa mnamo mwaka 1444 na kufariki dunia mnamo mwaka 1514 huko Italia ya Kati kwenye mji wa Urbino katika mkoa wa Marche karibu na pwani ya Bahari ya Adriatic kisha kufanya kazi Milan na Roma, ambapo alishirikiana na wasanii wakubwa kama Leonardo da Vinci na Michelangelo.

Bramante alihamasishwa na usanifu wa kale wa Warumi. Kazi zake zilionyesha ustadi wa kutumia kanuni za Vitruvian, hasa katika usawa wa mpangilio wa vipengele vya jengo, matumizi ya madoa (pilasters), matao, na kub (domes). Uwezo wake wa kutumia vipengele hivi kwa ubunifu mpya ulimtofautisha na wasanifu wa wakati wake.

Kazi maarufu ya Bramante ni Tempietto aliyoifanya mnamo mwaka 1502 katika San Pietro huko  Montorio, jijini Roma. Ingawa ni jengo dogo, linachukuliwa kuwa mfano kamili wa usanifu wa Renaissance. Tempietto lina umbo la duara, lina nguzo za Doric, na dome ya kifuvu, likiwa na ulinganifu wa ajabu. Hili lilikuwa jaribio la Bramante kuwasilisha upya hekalu la kale la Kirumi kwa muktadha wa Kikristo. Tempietto linaonekana kama jibu la usanifu kwa falsafa ya kidini na kisanaa ya Renaissance.

Hata hivyo wakati wa Papa Julius II Bramante aliteuliwa kubuni upya kanisa kuu la Mt. Petro mnamo mwaka 1506. Mpango wake wa awali ulihusisha umbo la msalaba wa Kigiriki, kwa kutumia dome kubwa katikati inayofanana na ile ya Pantheon ya Roma. Ingawa hakumaliza kazi hiyo kabla ya kifo chake, mpango wake uliathiri sana usanifu wa baadaye, na kazi hiyo ikaendelezwa na Michelangelo kwa mafanikio.

Donato Bramante anasalia kuwa mwasisi na kiungo muhimu katika mageuzi ya usanifu wakati wa Renaissance. Kwa kutumia misingi ya usanifu wa kale kwa njia mpya na bunifu, kwani  alileta sura mpya ya usanifu ambayo ilisisitiza uzuri wa kiakili na kihisia kwa wakati mmoja. Staili ya Renaissance, hasa kupitia kazi za Bramante, iliweka msingi wa usanifu wa kisasa, ikisisitiza uhusiano kati ya binadamu, nafasi, na uzuri wa kisayansi. Kazi zake hazikuchangia tu katika ustawi wa sanaa bali pia katika kuunda mazingira yanayoakisi maadili ya ubinadamu, utaratibu, na mwanga wa maarifa.




Saturday, May 10, 2025

Ifahamu Historia ya Mwanaharakati wa Tanzania; Mdude Nyagali

Mdude Nyagali
DoB: 25 Agosti 1987
PoB: Isongole, Ileje
Katika historia ya mataifa mbalimbali duniani, huwa kuna watu wanaojitokeza kama mashujaa wa fikra mbadala, wakijitoa kwa ajili ya kuhimiza haki, uwajibikaji, na demokrasia. Nchini Tanzania, jina la Mdude Nyagali, maarufu kama Mdude Chadema, limekuwa gumzo miongoni mwa wananchi wanaofuatilia siasa na masuala ya haki za binadamu. Mdude ni miongoni mwa wanaharakati wachache waliothubutu kusimama imara dhidi ya mamlaka na kukosoa hadharani mienendo ya serikali, licha ya changamoto na vitisho alivyokumbana navyo.

Mdude alizaliwa tarehe 25 Agosti 1987 katika kijiji cha Isongole, Wilaya ya Ileje, mkoani Mbeya. Alisoma katika shule za msingi Mkumbukwa na Msamba 1, kisha akaelekea Lubumbashi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, ambako alisomea masuala ya kompyuta. Baada ya kurejea Tanzania mwaka 2007, alijiunga na chama cha CHADEMA mwaka 2008 na kuanza kushiriki katika harakati za kisiasa akiwa kijana mwenye ari ya kuona taifa linatawaliwa kwa misingi ya haki na uwazi.

Katika miaka ya hivi karibuni, Mdude amejitokeza kuwa mmoja wa wakosoaji wakubwa wa serikali kupitia mitandao ya kijamii na mikutano ya kisiasa. Ameandika na kusema mambo mengi yanayolenga kuikosoa serikali, si kwa chuki binafsi, bali kwa nia ya kujenga taifa lenye uwazi na utawala wa sheria. Hii imemuweka kwenye hatari kubwa, ikiwa ni pamoja na kutekwa mwaka 2019, ambapo aliteswa na kutupwa akiwa na majeraha makubwa. Tukio hili lilisababisha mjadala mpana kuhusu usalama wa wanaharakati na nafasi ya uhuru wa kujieleza nchini Tanzania.

Licha ya changamoto hizo, Mdude hakuacha kusema. Aliendelea kushiriki katika siasa na kampeni mbalimbali, ikiwemo zile za uchaguzi wa serikali za mitaa, ambapo alikamatwa tena mwaka 2024 akiwa pamoja na viongozi wenzake wa CHADEMA, akiwemo Freeman Mbowe na Joseph Mbilinyi (Sugu). Kukamatwa kwake kulizua mijadala kuhusu matumizi ya nguvu dhidi ya wapinzani na namna vyombo vya dola vinavyotumika kisiasa.

Mbali na hayo, Mdude pia alikabiliwa na kesi mbalimbali, zikiwemo za tuhuma za dawa za kulevya mwaka 2020. Hata hivyo, kuna waliolitazama tukio hilo kama jaribio la kumharibia jina au kumdhibiti kisiasa, kutokana na misimamo yake ya ukosoaji.

Mdude anawakilisha kizazi cha vijana waliokataa kunyamaza mbele ya vitisho, wakiamini kuwa taifa bora hujengwa kwa fikra tofauti na usawa wa kila raia mbele ya sheria. Ameendelea kuwa sauti ya watu wasiokuwa na uwezo wa kujieleza hadharani, akisisitiza umuhimu wa haki, demokrasia, na utawala bora.

Kwa ujumla, maisha ya Mdude Nyagali ni mfano wa ujasiri na uzalendo. Ni kumbusho kwa Watanzania wote kuwa uhuru wa kujieleza si zawadi bali ni haki ya msingi ambayo inapaswa kulindwa kwa gharama yoyote. Katika mazingira ambayo maoni ya tofauti yanaonekana kama uasi, watu kama Mdude wanabeba dhamana nzito ya kulinda misingi ya demokrasia – hata pale inapowagharimu uhuru wao binafsi.

Monday, April 28, 2025

PAPA FRANCIS (1936-2025): Papa wa Kwanza, nje ya Ulaya tangu Karne ya 8; azikwa...R.I.P

Papa Francis (jina la kuzaliwa: Jorge Mario Bergoglio) alizaliwa tarehe 17 Desemba 1936 huko Buenos Aires, Argentina. Alikuwa Papa wa 266 wa Kanisa Katoliki, na alichaguliwa kuwa Papa tarehe 13 Machi 2013.


Papa Francis alifariki dunia tarehe 21 Aprili 2025 (Jumatatu ya Pasaka) saa 1:35 asubuhi kwa saa za Ulaya ya Kati, akiwa na umri wa miaka 88.

Alifariki kutokana na kiharusi kilichosababisha mshtuko wa moyo usioweza kurekebishwa. Alikuwa amehutubia hadhara kwa mara ya mwisho siku iliyotangulia, akitoa wito wa kusitisha mapigano huko Gaza.

Mazishi yake yalifanyika tarehe 26 Aprili 2025 katika Uwanja wa Mtakatifu Petro na kuhudhuriwa na zaidi ya watu 250,000 pamoja na wajumbe kutoka nchi zaidi ya 130. Alizikwa katika Basilika ya Santa Maria Maggiore mjini Roma, kwa ombi lake mwenyewe ili kupata mazishi ya kawaida na yasiyo na fahari nyingi.

Papa Francis (jina la kuzaliwa: Jorge Mario Bergoglio) alizaliwa tarehe 17 Desemba 1936 huko Buenos Aires, Argentina. Alikuwa Papa wa 266 wa Kanisa Katoliki, na alichaguliwa kuwa Papa tarehe 13 Machi 2013. Yeye alikuwa Papa wa kwanza kutoka Amerika ya Kusini, wa kwanza kutoka Bara la Kusini, na wa kwanza kutoka nje ya Ulaya tangu karne ya 8. Pia alikuwa Papa wa kwanza ambaye ni mtawa wa Shirika la Yesu (Jesuit).

Wednesday, April 23, 2025

Camerlengo Kadinali Kelvin Farrell ni nani?

Wakati dunia ikitoa machozi kwa kuondokewa na Papa Francis mnamo Jumatatu ya Aprili 21, 2025; kuna mtu asiyefahamika sana na maelfu ya wafuatiliaji wa masuala ya dini ya Katoliki mwenye asili ya Ireland aliyeishi muda mwingi nchini Marekani kabla ya kurudishwa makao makuu ya kanisa hilo jijini Vatican. 

Baada ya kutangaza kuwa Papa Francis “amerudi nyumbani kwa Baba” Kadinali Kevin Farell  ilikuwa ni habari mpya kabisa miongoni mwa wafuasi wa kanisa katoliki duniani kwamba kwa sasa atakuwa Camerlengo wa kanisa hilo ikiwa na maana kuwa atashikilia majukumu ya kuliongoza kanisa hilo mpaka atakapochaguliwa Papa mwingine. 

Papa Francis alimtangaza kuwa kadinali mnamo mwaka 2019 na kwamba kwa sasa Kadinali Farell atasalia katika nafasi hiyo “Apostolica Sedes Vacans ambapo neno "Apostolica Sedes Vacans" hutumika wakati wa kipindi cha mabadiliko baada ya kifo cha Papa au wakati ambapo Papa amejiuzulu, na wakati huu ni muhimu kwa ajili ya mchakato wa uchaguzi wa Papa mpya kupitia Konklave.

Pia Camerlengo Kadinali Kevin Farell anahudumu katika matukio yote kwa kipindi chote cha maombolezo.

Farell alizaliwa jijini Dublin mnamo mwaka 1947, alisoma katika Chuo Kikuu cha Salamanca nchini Hispania pia katika chuo kikuu cha Pontifical Gregorian jijini Rome.

Utumishi wake katika kanisa katoliki duniani alianza huduma za kiroho katika Chuo Kikuu cha Monterrey huko Mexico  pia katika Parishi ya Bethesda, Maryland.

Kadinali huyo mwenye umri wa miaka 77 sasa amehudumu katika makanisa ya katoliki kwa miaka 30 nchini Marekani, ambapo mwaka 2007 atangazwa kuwa Askofu wa Dallas hadi mwaka 2016 wakati ambao Papa Francis  alimtaka kurudi Vatican kama kiongozi wa Idara mpya ya Uangalizi wa Familia na ndio mwaka ambao alipandishwa hadi kuwa Kadinali. 

Mnamo mwaka 2023 Kadinali Farell alitajwa kama Camerlengo, pia alitangazwa na Papa Francis kama Rais wa Mahakama ya Juu ya Vatican City State na kuwa Rais wa Kamati ya Masuala ya Siri ya Kanisa Katoliki. 

Kadinali Farell atasimamia katika mkutano wa makadinali unaojulikana kama Konklave kwa ajili ya kumchagua Papa mpya wa kanisa hilo.

Vilevile kama ulikuwa hufahamu hili; Camerlengo anaweza kuchaguliwa kuwa Papa kama ilivyofanyika kwa Papa Leo wa XIII mnamo mwaka 1878 na Papa Pius XII mnamo mwaka 1939.

Camerlengo ina maana gani?

Camerlengo ni cheo cha juu kabisa katika Kanisa Katoliki kinachohusiana na uongozi wa Vatikani, Neno hili linatokana na maneno ya Kilatini "camerarius" (mtoa huduma au msimamizi wa chumba), na linahusiana na jukumu muhimu alilokuwa nalo Camerlengo katika kusimamia mali za Kanisa, hasa wakati wa kipindi cha mabadiliko baada ya kifo cha Papa au wakati ambapo Papa hayupo. 

Camerlengo ni kiongozi ambaye anachukua nafasi muhimu wakati wa kipindi cha mpito katika Kanisa Katoliki na kuhakikisha kwamba mchakato wa uongozi na uchaguzi wa Papa mpya unakwenda kwa usahihi.

Sunday, April 20, 2025

LILIAN KITHEE: Mwanamke Shujaa wa Gurudumu kutoka Kili Red Bikers, Kilimanjaro

 TASNIA YA UJASIRI NA UZALENDO: MWANAMKE AENDESHAE BAISKELI ZAIDI YA KILOMITA 1000 KUHAMASISHA MASUALA YA RED CROSS.

Katika jamii ya sasa inayokumbwa na changamoto mbalimbali za kijamii, kiuchumi na kiafya, kuna haja ya kuwa na watu wanaojitolea kwa hali na mali ili kuleta mabadiliko chanya. Mwanamke anapojitokeza kuendesha baiskeli zaidi ya kilomita 1000 kwa ajili ya kuhamasisha masuala ya Shirika la Msalaba Mwekundu (Red Cross), anatoa taswira ya ujasiri, kujitolea, na kuonesha kuwa mwanamke ana uwezo sawa wa kuleta mabadiliko katika jamii kama ilivyo kwa mwanamume.

Kwanza kabisa, tukio hilo linaonyesha nguvu ya mwanamke na usawa wa kijinsia. Kwa muda mrefu, jamii nyingi zimekuwa zikiamini kuwa kazi ngumu au shughuli zinazohitaji uvumilivu wa hali ya juu ni za wanaume pekee. Hata hivyo, mwanamke huyu anapovuka zaidi ya kilomita 1000 kwa baiskeli, anavunja minyororo ya dhana hizo potofu na kuhimiza jamii kutambua kuwa wanawake wana uwezo wa kufanya mambo makubwa yanayohitaji nguvu, maarifa, na dhamira thabiti.

Pili, hatua hiyo ni ishara ya uzalendo na moyo wa kujitolea. Kujiweka katika hali ya uchovu, hatari ya ajali, na changamoto za hali ya hewa ili kufikisha ujumbe wa msaada kwa jamii ni kitendo cha kujitoa kwa kiwango cha juu. Ni mfano bora kwa jamii kuhusu umuhimu wa kutoa mchango binafsi kwa ajili ya ustawi wa wengine, hasa wale walioko katika mazingira hatarishi kama waathirika wa maafa au migogoro.

Aidha, mwanamke huyu anatoa taswira ya uongozi wa kijamii. Katika harakati zake, si tu anahamasisha msaada kwa Red Cross bali pia anakuwa kielelezo cha mabadiliko. Anachochea mjadala wa kijamii kuhusu masuala ya kibinadamu na kuibua ari ya kujitolea kwa watu wengine. Uongozi huu wa kimyakimya lakini wenye nguvu, unaleta mabadiliko ya kweli ambayo mara nyingi hayawezi kupimwa kwa vyeo bali kwa athari.

Mbali na hayo, tukio hili linatoa taswira ya mshikamano wa kijamii. Mwanamke anapochukua jukumu kama hilo, anawakilisha siyo tu jinsia yake bali jamii nzima inayotaka kuona mabadiliko. Safari yake inaweza kuwa kichocheo cha watu kuungana kwa ajili ya kusaidia shughuli za kibinadamu kama vile kutoa damu, kusaidia waathirika wa maafa au kuelimisha jamii kuhusu afya.

Hitimisho, mwanamke anapojitokeza kuendesha baiskeli zaidi ya kilomita 1000 kuhamasisha masuala ya Red Cross anakuwa kielelezo hai cha ujasiri, usawa wa kijinsia, uzalendo, uongozi na mshikamano wa kijamii. Ni mfano wa kuigwa na sauti ya matumaini kwa jamii yenye kiu ya mabadiliko. Safari yake si tu ya baiskeli, bali ni safari ya matumaini, huruma, na mabadiliko ya kweli.

Tuesday, April 15, 2025

MMFA yapokea marekebisho ya Uwanja wa Railway Moshi; Meya Kidumo apewa maua yake

 

Marekebisho ya Uwanja wa Railway uliopo Njoro katika Kata ya Njoro, Manispaa ya Moshi ukifanyiwa marekebishwa kwa makatapira ikiwa ni mwendelezo wa kuinua vipaji vya soka kwa kuboresha miundombinu ikiwamo maeneo ya kuchezea yaani pitch. Meya wa Manispaa ya Moshi Injinia Zuberi Kidumo ndiye Diwani wa Kata hiyo ambako Uwanja wa Railway unafanyiwa marekebisho. (Credit to: Jabir Johnson/JAIZMELA).

Chama Cha Soka Manispaa ya Moshi (MMFA) mkoani Kilimanjaro kimepokea kwa shangwe kuu marekebisho yanayoendelea ya Uwanja wa Soka wa Railway.

Hatua ya kufanya marekebisho ya uwanja vya soka wa Railway yanatoa taswira kadhaa muhimu kuhusu maendeleo ya michezo, usimamizi wa miundombinu, na mwelekeo wa kijamii na kiuchumi katika mji.

Akizungumza uwanjani hapo Katibu wa MMFA Mwalimu Japhet Mpande amesema marekebisho yanaonyesha dhamira ya Manispaa ya Moshi kuboresha mazingira ya michezo kwa vijana na wakazi wake.

Mwalimu Mpande amesema yote yanaonesha kuwa Moshi inajitahidi kufikia viwango bora vya michezo na kuvutia mashindano ya kitaifa, pia inaweza kusaidia vijana wengi kujiingiza katika michezo kitaaluma au kupata ajira kupitia michezo.

………

Aidha Mwalimu Mpande ameongeza kuwa marekebisho ya viwanja mara nyingi huambatana na mpangilio mzuri wa mazingira ambapo yataongeza mvuto wa Manispaa ya Moshi kama sehemu inayojali mazingira na ustawi wa jamii.

Kwa upande wao wakazi wa Njoro uliopo uwanja wa Railway wamepokea kwa furaha na kutoa pongezi lukuki kwa Meya wa Manispaa ya Moshi Injinia Zuberi Kidumo ambaye ni Diwani wa Kata ya Njoro.

Aidha wakazi hao wameapa kuulinda uwanja huo ikiwamo tabia mbaya za udokozi, pia watu kukatisha uwanjani ili uendelee kuwa lulu kwa kata ya Njoro na Manispaa ya Moshi kwa ujumla.

…………….

Gharama za ukarabati huo bado hazijawekwa wazi mpaka utakapokamilika na taarifa rasmi kutolewa.

Viwanja bora vinaweza kuleta fursa za biashara ndogondogo (mfano wauzaji wa vyakula, vinywaji, mavazi ya michezo) na kuongeza mapato ya halmashauri kupitia kodi na matumizi ya viwanja kwa shughuli mbalimbali.

Uwanja wa Railway unafanyiwa marekebisho ikiwa ni takribani miongo minne kupita licha ya kwamba umekuwa ukitumiwa katika mashindano mbalimbali ikiwamo Zuberi Cup.















Sunday, April 13, 2025

Freeman Mbowe: Usiangalie siasa kama burudani; Siasa ni Maisha yako...


Safari ya Ukombozi wa Nchi yetu imekuwa ngumu, kwasababu watu hamko SERIOUS..Siasa imekuwa kama kitu cha mlipuko wakati wa Kampeni; kampeni zikiisha watu wanalegea, wanadhirika…tumekuwa na tabia kuhusudu na kuwaabudu viongozi, tunawasujudu viongozi; tunasahau sana watu wa Tanzania kuwa siasa ni maisha; Usiangalie siasa kama burudani…Siasa ni maisha yako; Viongozi wakeo ndio wanasababisha maisha uliyoko nayo leo…Sio Mungu; Wanasiasa na siasa wanaamua elimu yako leo; wanasiasa na siasa ndiyo imeamua ukaishia darasa la saba..

Freeman Mbowe; M/KITI Mstaafu wa Chadema.

Thursday, April 3, 2025

KIBONG’OTO: Kutoka kituo cha Utafiti wa Kahawa hadi Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi


Mpaka mwaka 1882 katika bara la Ulaya mtu mmoja kati ya watu saba alikuwa anakufa kwa ajili ya ugonjwa wa Kifua Kikuu ambapo tarehe 4 Machi 1882 Mjerumani wa Chuo Kikuu cha Gottingen Dkt. Robert Koch alitangaza kugundua kimelea kinachosababisha ugonjwa huo
  na kukipa jina la “Mycobacterium tuberculosis” MTB.

Hatua ya kubaini kinachosababisha ugonjwa wa kifua kikuu ilikuwa ni ugunduzi mkubwa kuwahi kutokea ulimwenguni kwani kwa miaka kenda rudi watalaamu mbalimbali waliketi chini kubaini kimelea kinachosababisha ugonjwa huo kama ni bakteria, protozoa, minyoo au ectoparasaiti.

Mwaka 1848 Mmishionari wa Kijerumani Johannes Rebmann aliandika rekodi ya kuwa mzungu wa kwanza kutoka barani Ulaya kuuona Mlima Kilimanjaro na baadaye walifuata wengine Richard Burton na  John Hanning Speke mnamo mwaka 1858 ambao walifanikiwa kuchora ramani ya Ziwa Tanganyika.

Mnamo mwaka 1884 kulifanyika Mkutano wa Berlin ambao ulikuwa maalum kwa ajili ya kuligawa bara la Afrika ambapo Tanganyika iliangukia mikononi mwa Ujerumani ambao walichukua na maeneo mengine kama Togo na Namibia. Walikaa Tanganyika kutoka miaka hiyo ya 1880 hadi waliposhindwa vita vya kwanza vya dunia mnamo mwaka 1919.

Tanganyika ilichukuliwa na Waingereza ambao walikaa hadi kupata uhuru mnamo tarehe 9 Desemba 1961; hivyo mambo mengi waliendeleza ikiwamo miradi mbalimbali ya kilimo;

Katika ardhi ya Tanganyika kanda ya kaskazini walianza utafiti wa mazao ya kahawa katika mkoa wa Kilimanjaro na Arusha; hata hivyo walivutiwa na eneo la Kibong’oto ambalo waliamua kuweka kituo chao cha utafiti wa zao la kahawa.

Hata hivyo baadaye walikuja kubaini wafanyakazi waliokuwa wakifanya kazi katika mashamba ya utafiti walikuwa wakikabiliwa na matatizo ya vifua na mapafu pia vikohozi visivyoisha na baridi hata wengine kupoteza maisha.



Zaidi anasimulia Dkt. Peter Daud ambaye ni Mtafiti wa Magonjwa ya Kuambukiza wa Hospitali ya Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto

Hospitali ya Kibong’oto ni hospitali yenye historia ndefu sana, Imekuwepo toka mwaka 1926 ilianzishwa kama kituo kidogo. Kilichoanzishwa na wakoloni, kilikuwa ni kituo cha utafiti wa mabo ya kahawa. Kwa nchi za Afrika Mashariki chini ya Mjerumani, Mjerumani alianzisha kama kituo kidogo cha utafiti wa kahawa; kadri muda uliuvyoenda wale waliokuwa wakifanya kazi katika mashamba ya kahawa wakaanza kuona, Kama wana ugonjwa ambao haueleweki; wanabanwa na mapafu, wanakohoa; kwasababu Mjerumani alikuwa anashirikiana na wenzao waliowaacha huko ndio wakajakugundua kuwa ulikuwa ni kifua kikuu. Ukiangalia kwenye memo walizokuwa wanaandikiana zilionyesha ni ugonjwa wa TB. Kwa hiyo wakahamisha kutoka kituo cha utafiti wa kahawa hadi kuwa sanatorium kuhudumia wagonjwa wanaopata ugonjwa kifua kifuu. Kwa hiyo ikaendelea hivyo mpaka tunafika kupata uhuru; pia tunafahamu kuwa baada ya vita ya dunia Tanganyika ilikuwa chini ya koloni la Waingereza; lakini wakaendeleza kuwa wanatibu wagonjwa wote waliokuwa chini ya makoloni ya Wajerumani na Waingereza. Baada ya kupata uhuru tunafahamu hali ya afya ilivyokuwa nchini; vituo vilikuwa vichache na vingine vilikuwa ni vya taasisi za kigeni; ilivyoendela hivyo; Kibong’oto ikaendelea kuwa ni hospitali ya kutibu wagonjwa wa Kifua Kikuu,” alisema Dkt. Peter Daud

Wakati inaanzishwa kama Sanatorium ya Kibong’oto mnamo mwaka 1926 Dkt. Norman Davies aliweka rekodi ya kwanza ya kuwa Mganga Mfawidhi akifuatiwa na Dkt. Allen Yatera. Mnamo mwaka 1978 Dkt. John Jacob Kifaruka alikuwa Mganga Mfawidhi hadi mwaka 1986, kisha Dkt. James Salekwa alihudumu katika wadhifa huo hadi mwaka 1992.

Dkt. Cathbert Kiwia alishika wadhifa huo hadi mwaka 1998 alipoukabidhi kwa Dkt. Liberate John Mleah ambaye alihudumu kwa miaka 10 hadi     mwaka 2014 akiweka rekodi ya kwanza tangu Tanganyika ipate uhuru kuwa Mganga mfawidhi aliyekalia kiti hicho kwa muda mrefu.

Dkt. Riziki Kisonga aliushika kwa miaka saba hadi tarehe 14 Oktoba mwaka 2021 pale Dkt. Leonard Subi alipokabidhiwa hadi sasa akiwa katika wadhifa wa Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali hiyo Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto.




“Jambo la Msingi katika Hospitali yetu ni kwamba hii ni hospitali ya kihistoria kwasababu ni moja ya chimbuko la sayansi ya matibabu ya  ugonjwa wa Kifua Kikuu nchini; Mwaka 1926 ndiyo ilianza kama hospitali ambapo ilianza kama kituo cha kutenga wagonjwa wa Kifua Kikuu. Lakini mwaka 1952 ikapandishwa hadhi na kuwa hospitali kamili ya Taifa ya Kifua Kikuu. Na ikumbukwe kwamba ilichukua takribani miaka 60 kugundua dawa za kutibu Kifua Kikuu tangu vimelea vya Kifua Kikuu vilivyogundulika mwaka 1882 na mwanasayansi mahiri wa Kijerumani Dkt. Robert Koch;” alisema Dkt. Leonard Subi

Mchango wa Hospitali  Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto baada ya uhuru wa Tanganyika mnamo mwaka 1961 ni mkubwa hasa ikizingatiwa wakati ule juhudi za kulikabilli janga hili la kifua kikuu lilikuwa bado katika kiwango cha chini ikilinganishwa na sasa

Sisi kama Hospitali ya Kibong’oto tunayo michango mikubwa sana na mpaka sasa tunaitwa Hospitali Maalumu ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto;  Hii kufuatia Tangazo la Serikali NA. 8828 la Novemba 2010 ambapo tulitangazwa kuwa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi. Na kwa muda mrefu tumekuwa tukitoa huduma za kimatibabu hususani matibabu ya kibingwa hususani katika magonjwa ya Kifua Kikuu lakini tangu tutangazwe sasa tumepanua wigo na kuyafikia magonjwa mengineyo;” aliongeza Dkt. Leonard Subi

Kibong’oto pia inatoa taswira ya athari za  Ukoloni katika sekta ya afya, kwani wakati wa utawala wa kikoloni hospitali hii ilikuwa pekee kwa ajili ya matibabu ya kifua kikuu licha ya kwamba baada ya uhuru serikali ya Tanzania ilijitahidi kufanya mabadiliko katika utoaji wa huduma za afya.

Mtafiti wa Magonjwa ya Kuambukiza wa Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto Dkt. Peter Daud anatupitisha katika eneo la vifaa na rekodi mbalimbali ambazo zilikuwa zikitumika wakati huo kabla ya mabadiliko makubwa yaliyofanywa na serikali ya Tanzania.
















Mbele yenu vitu mnavyoviona, hizi ni malikale sehemu ya kumbukumbu ya historia ya Hospitali ya Kibong’oto kama tunavyofahamu Hospitali imekuwepo tangu mwaka 1926 ikiwa inatoa matibabu ya kifua kikuu, ina maana kabla ya uhuru. Kwa hiyo hapa vitu tunavyoviona, hivi ni baadhi tu ya kumbukumbu za wagonjwa zinazoonyesha taarifa za wagonjwa waliowahi kutibiwa hapa kama inavyoonekana kuanzia mwaka 1923. Na hii hapa ndiyo rejista au leja ya wagonjwa wote waliokuwa wanafanyiwa upasuaji. Kama tunavyofahamu kabla ya dawa kuwepo, Hospitali ya Kibong’oto; ni ya kwanza Tanzania kufanya upasuaji wa mapafu; hii ni mojawapo ya kumbukumbu za wagonjwa waliokuwa wanafanyiwa upasuaji wa mapafu, moja ya sehemu ya matibabu ya Kifua Kikuu. Na hii kama inavyoonekana ni mihuri iliyokuwa inatumika kwamba mgonjwa alipokuwa akija; baada ya kuwa Daktari ameshampima kifua chake alikuwa anagonga muhuri sehemu alipoandika taarifa zake na sehemu ambayo imeharibika ya kifua. Na hiyo ilikuwa kwa ajili ya mwendelezo na kuonyesha wapi alipotoka na wapi anaelekea mgonjwa husika. Hiki pia kilikuwa ni kifaa kilichokuwa kikitumika katika upasuaji wa mapafu, kwasababu tunafahamu kwamba; wataalmu wa enzi hizo kabla ya uhuru walikuwa wakijaza hewa kwenye mapafu. Unajaza hewa kwa ajili ya kwenda kuua hivyo vijidudu kenye mapafu waliojificha. Kama unavyojua, upasuaji wa mapafu ni lazima uweze kuchana mbavu na hivi ni mojawapo ya vifaa vilivyotumika enzi za ukoloni kufanya upasuaji wa mapafu pia ni sehemu ya matibabu ya Kifua Kikuu. Kama tunavyoona vifaa vyote vilivyokuwa vikitumika katika kufungua mapafu, vingine vya sehemu za kujazia hewa na hewa hiyo ilikuwa inapimwa na mitambo. Mbele yenu huu ni mtambo, ulikuwa unatumika kwa wale wagonjwa waliokuwa wanakuja baada ya madaktari wameshawaona na vipimo vimefanyika kuwa wamejaa maji au usaha au kitu kingine ambacho kinahitaji kuvutwa na hii ilitumika wakati huo kufyonza, kwa sasa zipo za kisasa. Ilikuwa inatumika kuvuta damu, uchafu pia wakati wa upasuaji kwa mfano upasuaji wa mapafu, damu nyingi zilipokuwa zinatoka hii ilikuwa inatumika. Na hii ilikuwa sehemu ya mitungi ya Oksijeni, mgonjwa baada ya kufanyiwa upasuaji alikuwa anapelekwa katika chumba cha uangalizi maalum huku akiendelea kupata hewa ya Oksijeni. Hii hapa ni Mashine ya kuchomelea na sisi huku kwenye udaktari kuna sehemu huwa tunachomelea, wakati wa upasuaji unapokuwa unafungua kifua; ile mishipa midogo midogo ya damu inayovujisha damuili uwezekuona eneo lako la upasuaji vizuri; hii ndiyo mashine iliyokuwa inatumika kuchomelea kwa ajili ya kuziba ile mishipa ya damu isiweze kuchafua eneo ambalo daktari anafanyia upasuaji. Ni mashine ya zamani lakini bado ni mashine nzuri sana, kwa sasa bado inafanya kazi lakini kuna mashine za kisasa ambazo hatuwezi kutumia tena;” alifafanua Dkt. Peter Daud    

Baada ya Uhuru serikali ya Tanzania imeendelea kujikita katika mfumo wa afya wa kidemokrasia na unaohudumia watu wote wenye changamoto za kifua kikuu; Kibong’oto imekuwa mfano na alama muhimu ya utekelezaji  wa sera za afya na kuonyesha umuhimu wa kuhakikisha kuwa huduma za afya zinapatikana kwa watu wote bila kujali hali zao za kijamii na kiuchumi.      

Jina la Kibong’oto; yeyote Yule anayekuja hapa; ndiyo hospitali pekee inayotoa huduma kwa wagonjwa wa kifua kikuu ndiyo maana unaona sisi tunapokea wagonjwa wote nchi nzima. Na wengine wanatoka nchi za jirani hizi za maziwa makuu;  (Kibong’oto) imekuwa ni chachu ya kutoa matibabu kwa viwango vya kimataifa. Mgonjwa anayetibiwa hapa TB hata angeenda Ujerumani ataweza kutibiwa vilevile. Kwa hiyo kuna mwingine yuko Shinyanga, labda yupo Kazuramimba, Kigoma anavyoanza kujiona hapa nipo aua akawa anahisi naweza kuwa na TB; wengine wamekuwa wakipanda basi wenyewe, wanajileta wenyewe Kibong’oto na wanapata matibabu kasha kurudi majumabni kwao kuendelea na shughuli zao;” alongeza Dkt. Peter Daud    

Dkt. Peter Daud kama mwajiriwa katika Hospitali  Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto anafunguka kuhusu namna ambavyo mapambano dhidi ya Kifua Kikuu katika hospitali hiyo yalivyoacha kumbukumbu isiyofutika katika maisha yake pia yameacha matokeo chanya kitaifa na kimataifa.

Ilikuwa ni kuhamisha wagonjwa kutoka kwenye matibabu ya sindano na kuwahamisha moja kwa moja kwenye matibabu ya vidonge

Kwasababu tunafahamu hapo zamani tulikuwa tunatumia sindano kwani ilikuwa sehemu ya matibabu; kuna mgonjwa alikuwa anachomwa miezi nane na mwingine zaidi ya miezi nane; Unaweza ukafikiria kwamba kila siku ya Mungu anachoma sindano, sindano, sindano, sindano zaidi ya miezi nane lilikuwa siyo jambo la kawaida. Lakini kutokana na mabadiliko ya kiteknolojia sisi Kibong’oto tumekuwa sehemu ya kushiriki mabadiliko, tumeweza  kushiriki kushiriki kuwahamisha wagonjwa kutoka matumizi ya sindano hadi kwenye matumizi ya vidonge pekee. Hilo na jambo ambalo limenifurahisha sana, na sisi Kibong’oto ilikuwa ni sehemu ya mabadiliko na kuchangia kuwahamisha kutoka matumizi ya sindano hadi kwenye matumizi ya vidonge pekee;” alisema Dkt. Peter Daud    

Kwa upande wake Dkt. Subi anasisitiza kuwa mabadiliko makubwa yanayofanywa hospitalini hapo ikiwamo kukamilika kwa maabara ya Utafiti na Teknolojia ya Afya unaonyesha juhudi za kujenga uwezo wa utafiti na matumizi  ya teknolojia za kisasa katika kugundua na kutibu magonjwa.

Nikianza na matumizi ya ardhi; tumeandaa Master Plan. Kwamba hii ardhi tunaitumiaje? Kwasababu ni Hospitali ya Magonjwa Ambukizi; Master Plan yetu tumeigawanya katika maeneo, katika zones. Kwa mfano kuna zone ya maabara; maabara ya afya ya jamii, usalama wa kibaiolojia daraja la tatu;  Na maabara hiyo ina kazi zake maalum za uchunguzi wa magonjwa. Siyo maabara ya Kibong’oto peke yake lakini itatoa huduma za mapambano dhidi ya magonjwa ya kuambukiza hususani yale yenye umuhimu wa kipekee katika jamii; Lakini pia itatoa huduma za uchunguzi wa magonjwa mengine ya tiba ya kawaida; yakiwemo ya kuambukiza na yasiyokuwa ya kuambukiza. Na maabara ile ukiiangalia imejengwa na serikali makusudi. Na ndiyo uwekezaji mkubwa wa maabara katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; ambayo ina kila kitu kinachotakiwa duniani. Kwa maana kwamba, inaweza kuchunguza vimelea hatarishi duniani, vya ebola, Marburg, na vinginevyo; lakini inatumia teknolojia za kimolekyuli katika ugunduzi wa magonjwa. Lakini maabara hiyo pia inamwangalia binadamu kama yeye na pia itatumika katika tafiti mbalimbali;” alisema Dkt. Leonard Subi

Kwa ujumla Hospitali Maalum ya Taifa ya Magonjwa Ambukizi Kibong’oto inatoa taswira ya mabadiliko katika sekta ya afya, athari za ukoloni na juhudi za taifa katika kujenga mifumo ya afya baada ya uhuru pia inasimama kama kielelezo cha historia ya matibabu ya kifua kikuu na mchango wake  katika maendeleo ya afya nchini Tanzania.

Credit to: Johnson Jabir/JAIZMELA/ Kibong’oto Hospital; Barua Pepe: johnsonjabir@gmail.com



Monday, March 17, 2025

Godbless Lema: Wafanyabiashara wa Kichina wameleta ugumu kwa Wafanyabiashara Wazawa

 

Godbless Lema, mbunge wa zamani Jimbo la Arusha Mjini kwa tiketi ya Chadema; mnamo tarehe 21 Januari 2025 aliteuliwa rasmi kuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama hicho cha upinzani nchini Tanzania; baada ya Tundu Lissu kushika nafasi ya Uenyekiti. (Picha na MAKTABA/Jaizmela)

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimesema wafanyabiashara wazawa nchini wamedharauliwa vya kutosha kutokana na namna ambavyo serikali imewaruhusu raia wa China kushikilia sekta hiyo kwa kiwango kikubwa.

Akizungumza jijini Dar es Salaam hivi karibuni katika kampeni ya ‘Tone Tone’  ambayo inaendeshwa na Chadema kwa madhumuni ya kukusanya fedha kidogo kidogo kutoka kwa watanzania; Mjumbe wa Kamati kuu ya Chama hicho na Mbunge wa zamani wa Arusha Mjini Godbless Lema alisema wafanyabiashara wazawa, wanakutana na changamoto za upatikanaji wa mikopo na usaidizi wa kifedha, jambo ambalo linaweza kupunguza ushindani wao.

Lema aliongeza kuwa wafanyabiashara wa China wamekuwa wakiingiza bidhaa zao kwa bei nafuu ambazo zinaweza kushindana na bidhaa zinazozalishwa na wafanyabiashara wazawa, jambo ambalo limekuwa likisababisha sekta hiyo kwa wazawa kuwa dhaifu.

Katika kampeni ya Tone Tone Lema alisema wafuasi wa Chadema wanapaswa kujenga mfumo wa kukichangia chama ili kufanikisha malengo yake bila kutegemea msaada kutoka kwa serikali au vyanzo vya nje.

“Inafaa kuzingatia kwamba Michango inasaidia chama kusimamia haki za raia na kuhimiza utawala bora. Kwa mfano, Chadema, kama chama cha upinzani, kinapochangiwa fedha, kinaweza kuendesha kampeni za kuelimisha umma kuhusu haki zao, kutetea demokrasia, na kupigania mabadiliko ya kisiasa ili kuhakikisha usawa na haki kwa kila Mtanzania,” alisisitiza Mjumbe huyo wa Chadema

Viongozi wa Chadema wanaposimama na kuhamasisha michango ya Watanzania kwa chama hicho, wanatoa taswira ya chama kinachotegemea msaada wa raia ili kufanikisha malengo yake ya kisiasa, hasa katika mazingira ya ukosefu wa rasilimali kutoka kwa vyanzo vya kawaida kama vile serikali au wahisani wa nje.

Chadema sio wa kwanza, Katika kipindi cha Vita vya Vietnam, chama cha Viet Minh, kilichoongoza mapambano ya uhuru dhidi ya Ufaransa na baadaye Marekani, kilitegemea michango kutoka kwa wananchi na mashirika ya kiraia ili kudumisha harakati za vita na kuhamasisha jamii.

Tundu Lissu na wenzake sio wa kwanza, kufanya kampeni hiyo; Mahatma Gandhi alikuwa kiongozi muhimu katika harakati ya uhuru ya India dhidi ya utawala wa Uingereza. Fidel Castro na chama cha Maandamano ya Julai 26 walikusanya michango kutoka kwa wananchi ili kusaidia mapambano dhidi ya utawala wa Batista.

Pia Mwalimu Julius Kambarage Nyerere baada ya kupata uhuru, alihamasisha michango kutoka kwa wananchi ili kuendeleza maendeleo ya taifa na kujenga chama cha TANU;

Thomas Sankara, ambaye aliongoza mapinduzi ya Burkina Faso mwaka 1983, alihamasisha wananchi kutoa michango ili kufanikisha ajenda ya mabadiliko ya kijamii na kiuchumi. Sankara alisisitiza ushirikiano wa wananchi na akahamasisha mchango wa kifedha, mali, na rasilimali nyingine kwa ajili ya kupambana na umasikini, kupigana na rushwa, na kuboresha ustawi wa jamii.

Hivyo basi; kimataifa, viongozi wa Chadema wanapohamasisha michango, wanaweza kuonesha kwamba chama hicho kinapigania demokrasia ya kweli na utawala bora, na kuwa na msaada wa watu wa kawaida ikiwa ni ishara ya kuungwa mkono na wananchi dhidi ya mifumo ya kisiasa isiyokuwa na uwazi.

Hii pia inaweza kuvutia uangalizi kutoka kwa mashirika ya kimataifa na wadau wa demokrasia na haki za binadamu, kwani michango ya wananchi inaweza kutafsiriwa kama ishara ya ushiriki wa wananchi katika mchakato wa kisiasa, jambo linalothaminiwa kimataifa.

MWISHO