Baada ya kuchaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki duniani Papa Leo XIV ameanza rasmi kuishi katika nyumba ya kipapa iliyopo Vatican.
Wengi walikuwa na maswali kuhusu suala hilo kama atafuata
nyayo za mtangulizi wake Papa Francis aliyekuwa akiishi pasipo anasa katika
Nyumba za Wageni za Vatican.
Papa Francis aliweka rekodi ya kuwa papa wa kwanza kukataa
kuishi katika Kasri la Vatican baada ya miaka 143 ambapo alichagua kuishi Santa
Marta Motel, Vatican.
Papa Leo XIV amechagua kuishi katika Kasri la Kitume la
Vatican (Vatican Apostilic Palace) kwa ajili ya kuendelea na huduma yake
kulisimamia Kanisa Katoliki duniani.
Vatican Apostolic Palace ni jengo ambalo lilisanifiwa na
kuanza kujenga mnamo karne ya 15 kwa usanifu wake Donato Bramante katika muundo
wa Reinaissance.
Kipindi hiki cha
Renaissance kilikuwa cha mabadiliko makubwa ya kisanaa, kielimu, na kifalsafa
kilichoanzia katika ardhi ya Italia kwenye karne ya 14 na kuenea Ulaya nzima
hadi karne ya 17.
Katika sanaa ya majengo, kipindi hiki kilihama kutoka kwa
usanii wa kati wa kighorofa yaani Gothic na kuzingatia upya kanuni za uzuri,
usawa, na mantiki zilizoasisiwa na Warumi na Wagiriki wa kale.
Moja ya majina makubwa katika kipindi hiki ni msanifu wa jengo
la sasa la Vatican Apostolic Palace; Donato Bramante, ambaye alichangia sana
kuasisi na kuendeleza staili ya usanifu ya Renaissance ya juu.
Vatican Apostolic Palace imeundwa na vyumba 1000 ikiwamo
sehemu ya kukaa, kulala na kliniki ya dawa. Jengo hili pia lina Kanisa la
Sistina ambalo ni mojawapo ya majengo mashuhuri zaidi duniani, hasa kutokana na
uzuri wa sanaa yake ya ndani, hasa michoro ya dari inayoonyesha Hukumu ya Mwisho iliyochorwa na
Michelangelo.
Papa Leo XIV anajitokeza kama kiongozi mwenye maono makubwa
ya kurejesha Kanisa katika misingi yake ya asili: kiroho safi, maadili mema, na
uaminifu wa ndani kwa injili ya Kristo.
Dunia ya sasa inakabiliwa na changamoto nyingi, kuanzia
mmomonyoko wa maadili, maisha ya kiroho kupoa, hadi migogoro ya ndani ya
taasisi ya Kanisa.
Hali hii inamtia moyo Papa Leo XIV kuchukua hatua madhubuti
za kufufua maisha ya kiroho na kimaadili miongoni mwa waumini, pamoja na
kufanya mageuzi ya ndani ya Kanisa yanayolenga uwazi, usafi wa utume, na kujibu
hitaji la kizazi cha sasa.
Tukirejea kwake; Donato Bramante alizaliwa mnamo mwaka 1444
na kufariki dunia mnamo mwaka 1514 huko Italia ya Kati kwenye mji wa Urbino
katika mkoa wa Marche karibu na pwani ya Bahari ya Adriatic kisha kufanya kazi
Milan na Roma, ambapo alishirikiana na wasanii wakubwa kama Leonardo da Vinci
na Michelangelo.
Bramante alihamasishwa na usanifu wa kale wa Warumi. Kazi
zake zilionyesha ustadi wa kutumia kanuni za Vitruvian, hasa katika usawa wa
mpangilio wa vipengele vya jengo, matumizi ya madoa (pilasters), matao, na kub
(domes). Uwezo wake wa kutumia vipengele hivi kwa ubunifu mpya ulimtofautisha
na wasanifu wa wakati wake.
Kazi maarufu ya Bramante ni Tempietto aliyoifanya mnamo mwaka
1502 katika San Pietro huko Montorio,
jijini Roma. Ingawa ni jengo dogo, linachukuliwa kuwa mfano kamili wa usanifu
wa Renaissance. Tempietto lina umbo la duara, lina nguzo za Doric, na dome ya
kifuvu, likiwa na ulinganifu wa ajabu. Hili lilikuwa jaribio la Bramante
kuwasilisha upya hekalu la kale la Kirumi kwa muktadha wa Kikristo. Tempietto
linaonekana kama jibu la usanifu kwa falsafa ya kidini na kisanaa ya
Renaissance.
Hata hivyo wakati wa Papa Julius II Bramante aliteuliwa kubuni
upya kanisa kuu la Mt. Petro mnamo mwaka 1506. Mpango wake wa awali ulihusisha
umbo la msalaba wa Kigiriki, kwa kutumia dome kubwa katikati inayofanana na ile
ya Pantheon ya Roma. Ingawa hakumaliza kazi hiyo kabla ya kifo chake, mpango
wake uliathiri sana usanifu wa baadaye, na kazi hiyo ikaendelezwa na
Michelangelo kwa mafanikio.
Donato Bramante anasalia kuwa mwasisi na kiungo muhimu katika
mageuzi ya usanifu wakati wa Renaissance. Kwa kutumia misingi ya usanifu wa
kale kwa njia mpya na bunifu, kwani alileta sura mpya ya usanifu ambayo
ilisisitiza uzuri wa kiakili na kihisia kwa wakati mmoja. Staili ya
Renaissance, hasa kupitia kazi za Bramante, iliweka msingi wa usanifu wa
kisasa, ikisisitiza uhusiano kati ya binadamu, nafasi, na uzuri wa kisayansi.
Kazi zake hazikuchangia tu katika ustawi wa sanaa bali pia katika kuunda
mazingira yanayoakisi maadili ya ubinadamu, utaratibu, na mwanga wa maarifa.
0 Comments:
Post a Comment