Saturday, October 5, 2024

Kahawa Festival 2024 kusaidia wakulima kupata mbinu mpya

Mkurugenzi wa Bodi ya Kahawa Tanzania (TCB), Primus Kimaryo, akitoa maelezo kuhusu kahawa kwa mgeni rasmi wa ufunguzi wa Kahawa Festival 2024 msimu wa tano mnamo Septemba 4, 2024; Mkuu wa Wilaya ya Moshi James Kaji. Ufunguzi huo umefanyika katika Kiwanda cha Kukoboa Kahawa (Coffee Curing) mjini Moshi. (Picha na Dani Kazili/ JAIZMELA)


Mkurugenzi wa Bodi ya Kahawa Tanzania (TCB), Primus Kimaryo, amesisitiza umuhimu wa uanzishwaji wa matamasha ya kahawa katika kusaidia wakulima wa zao hilo kupata mbinu bora za kilimo.

Akizungumza katika uzinduzi wa Kahawa Festival 2024, mnamo Septemba 4, 2024  Kimaryo alieleza kuwa matukio haya ni fursa ya kipekee kwa wakulima kujifunza na kuboresha uzalishaji wao.

Kimaryo alisema kuwa matamasha yanatoa jukwaa kwa wakulima kukutana na wataalamu wa kilimo, ambapo wanaweza kupata mafunzo kuhusu mbinu za kisasa za kilimo, usimamizi wa mashamba, na teknolojia mpya.

"Tunaamini kuwa elimu ni msingi wa maendeleo. Wakulima wanapojifunza mbinu bora, wanakuwa na uwezo wa kuongeza uzalishaji na kuboresha ubora wa kahawa yao," alifafanua.

Alisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya wakulima, serikali, na wadau wengine katika sekta ya kahawa. "Tunaweza kufanikisha mabadiliko makubwa kwa kushirikiana. Matamasha haya ni fursa ya kuungana na kujadili changamoto na fursa zinazokabili sekta ya kahawa," alisema Kimaryo. 

Kimaryo aliongeza kuwa matamasha yanaweza kusaidia kuboresha soko la kahawa nchini. 

"Kwa kutoa elimu na mafunzo, wakulima wataweza kuzalisha kahawa bora, ambayo itavutia wanunuzi na kuongeza thamani ya bidhaa zetu katika masoko ya ndani na nje," alisema. 

“Uanzishwaji wa matamasha ya kahawa ni hatua muhimu katika kusaidia wakulima kupata mbinu bora na kuboresha uzalishaji wa kahawa nchini.

Kimaryo, alisisitiza kuwa elimu na ushirikiano ni muhimu katika kuimarisha sekta ya kahawa na kuhakikisha kuwa wakulima wanapata faida inayostahili kutokana na kazi zao.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kahawa Festival, Denis Mahulu, alisema idadi ya watu wanaoshiriki kuonyesha bidhaa zinazotokana na zao la kahawa inazidi kuongezeka kila mwaka ambapo washiriki kutoka maeneo mbalimbali, wamekuwa wakishiriki kuonyesha ubunifu na ubora katika bidhaa zao.

Mahulu alisema kwamba ongezeko la washiriki hao ni dalili nzuri ya ukuaji wa sekta ya kahawa, kupitia Tamasha la Kahawa Festival-2024, wakati tamasha hilo  linaanzishwa mwaka 2019 washiri walikuwa 25 na kwa sasa washiriki wako zaidi ya 40, ambapo tamasha hilo, linatoa fursa kwa wakulima na wazalishaji wa kahawa kuungana, kubadilishana mawazo, na kujifunza mbinu bora za kilimo na usindikaji.

Mgeni rasmi wa ufunguzi wa Kahawa Festival 2024 alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Moshi James Kaji ambaye alisisitiza uanzishwaji wa mashindano ya michezo kama vile riadha ili kuimarisha unywaji wa kahawa na kupanua wigo wa zao hilo kwa kila mdau nchini na kimataifa.

Kauli Mbiu ya Kahawa Festival 2024 inasema; “Ushirikiano wa dau kwa Pamoja katika uendelezaji wa tasnia ya Kahawa.”

CREDIT TO: Johnson Jabir, (JAIZMELA Correspondent.)






0 Comments:

Post a Comment