Wednesday, August 28, 2024

Wamajumuhi wa Afrika mjini Moshi waadhimisha kuzaliwa kwa Marcus Garvey (1887-1940)

Marcus Garvey (1887-1940)

 Wamajumuhi wa Afrika mjini Moshi wameadhimisha miaka 137 ya kuzaliwa kwa Mwanaharakati wa Haki za Watu Weusi Marcus Garvey.

Maadhimisho hayo yamefanyika mjini Moshi mkoani Kilimanjaro mnamo Agosti 17, 2024 yakiwaleta pamoja wamajumuhi wengine kutokaTanzania na  Amerika hususani Jamaica, Trinidad & Tobago na Canada.

Akizungumza katika ufunguzi wa maadhimisho hayo mwenyeji wa Wamajumuhi hao Rasta Gasper Shirima anasema wanaendelea kushikilia falsafa za Garvey licha ya kukabiliwa na changamoto lukuki ikiwamo ukosefu wa maarifa kwa watu wa Afrika Mashabiki kuhusu umajumuhi wenyewe wa Kiafrika.

Rasta Shirima anaongeza kusema serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imejitahidi kuwapa eneo katika Manispaa ya Moshi kwa ajili ya kutoa maarifa hayo Bure licha ya mwendo wa kinyonga katika kubadilisha mitaala ya Elimu na kuweka umajumuhi wa Kiafrika.

Suala la waafrika walio nje ya nchi zao wanaofahamika kwa jina la Diaspora lilikuwa mjadala mrefu huku wakitaka kujua hatua zimefikia wapi kuwafikia viongozi wa serikali na wabunge katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili kutoa mwanya wa kubadilisha Sheria.

Watanzania wenyewe wanasemaje kuhusu umajumuhi wa Kiafrika na jamii inawatazamaje wanapojifunza.

Kwa upande wake Mtaalamu wa Tiba Asili kutoka nchini Jamaica Michael Jocko amewataka watanzania kuwa na nidhamu ya chakula ili kutunza Afya zao na kuwa na maisha marefu.

Marcus Garvey alizaliwa Jamaica mwaka 1887. Kwamba mweusi huyu wa ngozi aliyewataka Waafrika kujivunia Uafrika wao, alizaliwa katika bara la Amerika Kusini ni kielelezo cha historia chungu ya ujenzi wa ubepari. Ubepari wa Ulaya ulijengwa katika msingi wa uporaji wa ardhi kutoka kwa wenyeji wa Amerika, na uporaji wa nguvu-kazi kutoka Afrika. Hadi kufikia mwaka 1800, mathalani, idadi ya wazungu kisiwani Jamaica ilikuwa ni ishirini na moja elfu huku Waafrika waliogeuzwa watumwa wakiwa ni laki tatu. “Watumwa” hao walitumika kuzalisha miwa/sukari ambayo ilisafirishwa kwenda Uingereza.

Wakati Garvey anazaliwa, biashara ya utumwa ilikuwa imekomeshwa huko Amerika, lakini Waafrika hawakuonekana kama binadamu kamili: waliendelea kubaguliwa, kunyanyaswa na kunyonywa.

Garvey aliuona ubaguzi huo tangu akiwa mdogo nchini Jamaica. Haishangazi basi, mapambano yake yalikuwa ni ya kupinga ubaguzi wa rangi. Baada ya kusafiri na kufanya kazi katika nchi mbali mbali za Karibiani, na baadaye Uingereza, Garvey alikwenda Marekani mwaka 1916. Ni huko Marekani ambako taasisi aliyoianzisha, ijulikanayo kama UNIA (Universal Negro Improvement Association) ilipata wanachama na wafuasi wengi.


























0 Comments:

Post a Comment