Ukweli na Kuheshimiana ni kiini ujenzi wa jamii zetu

Ulimwenguni kwa sasa kumejaa habari potofu na upotoshaji, ni muhimu kuhakikisha kwamba ukweli na kuheshimiana vinakuwa kiini kwa ujenzi wa jamii zetu.

Mapambano dhidi ya Habari za Uongo hayapaswi kukoma

Habari za uongo, habari za uongo zinazosambazwa kwa lengo la kumdhuru mtu au jambo fulani, huifanya jamii kuwa na sintofahamu. Zinaweza kutumika kwa madhumuni ya kiitikadi, kisiasa au hata uhalifu, kama vile ulaghai mtandaoni unaolenga kuiba data ya kibinafsi.

Utandawazi na Athari zake katika Uandishi wa Habari

Katika jamii yetu ya kisasa, ambapo habari ziko kila mahali na zinaweza kupatikana kwa kila mtu, mara nyingi ni ngumu kutofautisha kati ya vyanzo vya kuaminika na habari bandia.

Uandishi wa Habari nguzo msingi mkuu kwa ujenzi wa jamii inayojitambua

JAIZMELA blog ni miongoni mwa vyanzo vya habari, zilizochakatwa kwa kuzingatia miiko ya uandishi wa habari.

Mila na Desturi ni nguzo muhimu

Mila na desturi ni nguzo muhimu sana katika utamaduni wa jamii yoyote ile; mila ni sawa na sheria zisizoandikwa. Mila ni taratibu za maisha na mwenendo zinazofuatwa na jamii fulani katika utendaji kulingana na historia na utamaduni wao. Mila zinatambulisha maadili ya jamii husika, huelezea namna jamii inavyoendesha mambo yake.

Sunday, June 30, 2024

Mikopo ya Halmashauri kuanza kutolewa tena Julai 1, 2024

Diwani wa Kata ya Korongoni, Moshi, Bi. Heavenlight Kiyondo akiwa na mjukuu wake nyumbani kwake. Diwani huyo amekuwa mstari wa mbele kuwahamasisha wanawake na vijana kwenda kukopa katika Halmashauri mikopo isiyo na masharti magumu ili kujiepusha na mikopo itakayowapeleka kwenye mateso wakati wa kuirudisha. Julai 1, 2024 Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilisema itaanza tena kutoa mikopo hiyo katika halmashauri zote nchini. (Picha na JAIZMELA).


Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa, sura ya 290 ilifanyiwa marekebisho mwaka 2018 ili kuweka masharti kwa Halmashauri zote nchini kutenga fedha kwa ajili ya mikopo kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Kufuatia marekebisho hayo Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) ilitunga kanuni zinazoanisha masharti ya utozaji na usimamizi wa mikopo inayotolewa na Halmashauri kwa vikundi hivyo.

Kanuni ya 4 ya Utengaji wa Fedha za Mikopo inamweka bayana Halmashauri inatakuwa na wajibu wa kutenga asilimia 10 ya Mapato yanayotoka katika vyanzo vyake vya ndani kwa ajili ya kutoa mikopo kwa vikundi  vya wanawake asilimia 4, vijana asilimia 4, na watu wenye ulemavu asilimia 2.

Mnamo Aprili 13,2023 katika Bunge la 12 Waziri Mkuu wa Jamhuri Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa alitangaza usitishwaji wa mikopo hiyo ili kupisha utaratibu mwingine wa utoaji wa mikopo.

Baada ya mwaka mmoja, mnamo Aprili 16, 2024 Waziri wa TAMISEMI Mohammed Mchengerwa alitangaza kurejesha kwa mikopo hiyo wakati akisoma bajeti yake ya mwaka 2024/25.

Jumatatu ya Mei 13, 2024 Naibu Waziri TAMISEMI Zainab Katimba wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalum Josephine Gezabuke aliwaondoa hofu wanawake, vijana na watu wenye ulemavu na kwamba mikopo hiyo rasmi itaanza kutolewa Julai Mosi 2024.

Katimba alisema Rais Samia Suluhu Hassan ameridhia kutolewa tena mikopo hiyo, bayana sababu iliyofanya isitishwe kuwa marejesho kwa vikundi vilivyokuwa vikidaiwa yalikuwa yanaendelea.

Shilingi bilioni 227.96 zinatarajiwa kutolewa kwa vikundi hivyo nchi nzima huku shilingi bilioni 63.67 zikiwa ni fedha za marejesho kwa mikopo ilitotolewa kabla ya kusimamishwa.

Dkt. Nchimbi anavyowatazama Tundu Lissu, Mbowe


Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi  (CCM) Taifa; Dkt. Emmanuel Nchimbi katika mkutano wa Hadhara katika mji wa BomaNg'ombe wilayani Hai Juni 4,  2024 (Picha na Jabir Johnson/JAIZMELA)


Katika miongoni ya mikutano ya hadhara iliyowastaajabisha wengi na hawakutegemea kama ingalikuwa hivyo ni ule wa Juni 4, 2024 uliofanyika katika mji wa Bomang;’ombe, wilayani Hai mkoani Kilimanjaro.

Mkutano huo ulihutubiwa na Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ikiwa ni siku ya kwanza ya ziara yake mkoani Kilimanjaro alikopita kuzungumza na watanzania kuhusu mambo mbalimbali yanayofanywa na chama hicho.

Kiini cha makala haya ni pale hasa alipogusia suala la demokrasia ndani na nje ya Tanzania. Dkt.Nchimbi alivuta usikivu wa watanzania waliomiminika hapo wake kwa waume kumsikiliza na wengine walipata fursa ya kuwasilisha kero zao.

Alianza hivi, ““Hivi ninyi mkiamka na kukuta mtu anafagia uwanja wa nyumba yao unakasirika? Ukiwa na nguo chafu halafu ukamkuta mtu amezifua na kuzianika unakasirika,”

Dkt. Nchimbi anavuta funda la mate na kuendelea, “Tundu Lissu na Mbowe wanakisaidia CCM kufagia uwanja, wanatufulia nguo, tunawashukuru sana kwa kututendea wema huo wa kufanya kazi za CCM ya kuitangaza demokrasia ya nchi yetu  hakuna sababu ya kugombana nao mnapokutana nao.”

Hapo ndipo mwanasiasa huyo mkongwe aliyelelewa vema ndani ya chama hicho na kufikia kuwa Katibu Mkuu wa CCM aliponifanya nirudie hotuba na maneno ya mwasisi wa chama hicho ambaye ni Baba wa Taifa la Tanzania Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika kitabu chake cha Binadamu na Maendeleo alichokiandika mnamo mwaka 1974.

Mwalimu Nyerere aliandika, “`Kuna mambo mawili ya lazima katika demokrasia, ukiyakosa hayo demokrasia hakuna. La kwanza: Ni kwamba kila mtu lazima aweze kusema kwa uhuru kabisa na maneno ya kila mtu lazima yasikilizwe.

Nyerere aliongeza, “Hata kama maneno ya mtu huyo hayapendwi kiasi gani, au walio wengi wanamdhania amepotoka kiasi gani si kitu, kama mtu anapendwa kwa wema wake au hapendwi kwa visa vyake hayo yote si kitu.”

Pia Mwalimu Nyerere alisisitiza, “Majadiliano lazima yaruhusiwe kuendelea kwa uhuru kabisa, hiyo ni sehemu ya maana ya uhuru wa mtu binafsi.”

Dkt. Nchimbi aliwavutia wengi sana katika hotuba yake hiyo kwa watanzania miongoni mwa maneno yake yatakayokumbukwa kuhusu demokrasia katika taifa la Tanzania.

Katibu Mkuu huyo alisisitiza sana, ndani na nje ya chama kutogombana na wapinzani kwani kwa namna moja au nyingine ni kumwangusha Rais Samia Suluhu Hassan katika majukumu yake ya kuijenga Tanzania mpya inayojali demokrasia na uhuru wa kila mmoja pasipo kuvunja sheria.

“Rais Samia amedhamiria kusimamia misingi ya Chama chetu ya kuimarisha  demokrasia ndani ya chama na nje ya chama chetu. Wana-CCM wawe na haki ya kuchagua na kuchaguliwa  na haki hiyo inapatikana bila masharti yoyote,” aliongeza Dkt. Nchimbi.

Dkt. Nchimbi aliweka bayana kuwa wapinzani wakuu wa CCM ambao ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wangekuwa na wanahitaji kulipwa angewalipa kiasi cha kutosha cha fedha kwa kuendelea kuitangaza demokrasia ndani na nje ya nchi.

“Wapinzani wanatusaidia sana kufanya kazi, ya kuiambia dunia kwamba Tanzania kuna demokrasia ya kutosha wakati mwingine wanafanya kazi yetu, Mimi nikiwaona Freeman Mbowe na Tundu Lisu wakitoka jasho kwenye maandamano moyoni mwangu nasema mnatusaidia kazi Baba!!na wangekuwa wanahitaji malipo ya kufanya hiyo kazi Walahi ningewalipa, ingekuwa wanahitaji malipo ningewwalipa.

Madhumuni ya ziara ya Dkt. Nchimbi mkoani Kilimanjaro ni; Kuangalia Utekelezaji wa Ialni ya CCM, Ilani ni mkataba kati ya Wananchi na Chama, tulipofanya uchaguzi mwa 2020 yako malengo ya miaka mitano ya CCM iliyoyaweka.

Imeandikwa na Jabir Johnson

+255 693 710 200

TFF yatakiwa kulipa hadhi soka la Mitaa, Viwanja nyasi bandia

Soka ni miongoni mwa michezo maarufu ulimwenguni na unaopendwa na watu wengi, kazazi cha Karne ya 21 hakiwezi kuwasahau Cristiano Ronaldo wa Ureno na Lionel Messi wa Argentina.

Nyota hawa Wawili wamekuwa katika viwango vya juu siku zote katika maisha Yao ya soka lakini Jambo moja kubwa ambalo wengi huenda hawalipi uzito zaidi ya kuangalia namna wanavyovuna mabilioni ya Shilingi kutokana na kutandaza soka lenye mvuto ni kwamba wote Wawili walitoka katika familia maskini.

Cristiano Ronaldo alitoka katika familia ya baba mlevi kupindukia ambaye alifariki Dunia kutokana na ulevi wake, mama yake alikuwa akifanya kila jitihada kuhakikisha mwanaye anapata fursa ya kucheza mpira na ndoto ikawa kweli.

Lionel Messi alifahamika kwao kwa jina moja la Kiroboto au kwa kihispaniola La Pulga kutokana na ufupi wa kimo licha ya kuzaliwa akiwa na changamoto ya mgongo lakini wazazi wake hawakukata tamaa kumkuza katika soka na ndoto ikawa kweli alipotua katika Akademi ya La Masia.

Mifano hiyo miwili inaweza kuwa mfano mzuri kwa watoto wa Kitanzania ambao wengi wanatoka mazingira duni ambayo hata kununua kiatu cha mpira ni changamoto.

Katika Manispaa ya Moshi kumekuwa na Mashindano ya kandanda ya Mtaa yaliyoasisiwa katika Viwanja vya Railway kwenye Kata ya Njoro ambako Diwani na Mstahiki Meya wa Manispaa hiyo Injinia Zuberi Abdallah Kidumo anatokea.

Mashindano hayo maarufu ya kandanda iliyopewa jina la Zuberi Cup Tournament hufanyika baada ya msimu wa soka unaomalizika mwezi Mei kila mwaka unapoisha hivyo wakazi wengi wa Mkoa wa Kilimanjaro hupata fursa ya kujionea vipaji vya kandanda.

Baada ya msimu mitatu kuchezwa mwaka huu tena yameanza ambapo kipute mwaka huu kinashiriki timu 25 huku zawadi ya bingwa itakuwa shilingi milioni tatu za Kitanzania ikiwa ni rekodi ya juu kuwahi kutokea katika michuano ya soka mkoani Kilimanjaro.

Mnamo Juni 16, 2024 katika ufunguzi wa Zuberi Cup Tournament Mgeni rasmi alikuwa Mwasisi wa Michuano ya Kandanda mitaani maarufu Ndondo Cup Shaffih Dauda.

Katika ujumbe wake kwa Watanzania na wapendwa kandanda nchini alitaka Mashindano hayo ya kandanda yanayofanyika katika Mitaa yatambulike rasmi kama sehemu ya kudaka vipaji na kukuza soka nchini.

"Sisi kama wadau wa Mpira wa Mtaani tunaomba mtutambie rasmi sio tuje kuchukua vibali na kutuacha, mtushike mkono, mtutambue jitihada zetu na sisi tupo hapa kwa ajili ya kuwasapoti nyie, hatupo hapa kwa ajili ya kuwatengenezea labda ushindani tupo hapa kwa ajili ya kusapoti mambo mazuri," alisema Dauda.

Dauda aliwataka waratibu wa Mashindano kama hayo kote nchini kuungana pamoja na kutengeneza Taasisi itakayokuwa inatambulika kwa ajili ya kandanda la mtaani ili kuongeza ushawishi nchini.

"Kuna Jambo ambalo naliota siku zote sisi kama waandaji wa Mashindano nchini tuwe na umoja wetu, tutengeneze umoja kwenye mikoa yote ambayo Mashindano yanafanyika uswahilini. Na sisi tuwe na sauti moja kuzungumza kwa pamoja na ikiwezekana tuwe na mipango ya kuboresha," aliongoza Dauda.

Aidha Mwasisi huyo na mchambuzi wa kandanda nchini aliliomba Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kutumia mwanya wa serikali kusamehe Kodi katika vifaa vya Taasisi za serikali kupeleka kwa Miradi ya Viwanja vya Nyasi Bandia katika kila wilaya kote nchini.

"Hivi viwanja ambayo viko huku mtaani chini kupitia kwenye uongozi wenu nafikiri kuna haja ya kuviangalia kwa Jicho lingine na kutumia fursa ambayo Mheshimiwa Rais ameitoa ya kutoa wave ya Kodi ya majani bandia, na huku mtaani, huku uswahilini hatuhitaji hii natural grasses, tunakuhitaji artificial grasses ndio zinatufaa zinakaa muda mrefu katika mazingira yetu," alisisitiza.

Kwa upande wake Mstahiki Meya wa Manispaa ya Moshi Injinia Zuberi Kidumo alisema mchezo wa kandanda unapendwa na watu wengi ulimwenguni hivyo juhudi ni vema kuongeza katika kuyafanya Mashindano ya Uswahilini kuwa sehemu ya ajira, burudani na fursa kwa wachezaji kuipandisha viwango vyao.

Awali Dauda katika ufunguzi alisifu juhudi za Rais Samia Suluhu Hassan katika kuunga mkono sekta ya Michezo nchini.

"Sisi sote ni mashahidi, Ningeomba kwa pamoja tumpigie makofi kuonyesha appreciation kwake kwa kutubeba maana yake ni kwamba amekuwa akihamasisha timu zetu, amekuwa akipambana, Afcon inakuja hapa kwetu ni fursa kubwa kwetu sisi kama Watanzania na kwa vijana ambao wanapata nafasi ya kucheza timu ya taifa baadhi lakini ni jambo kubwa," alisema Dauda.

Imeandikwa na:
Jabir Johnson
+255 693 710 200