Header Ads Widget

Responsive Advertisement

RON W. DAVIS: Namna alivyokuwa kocha wa Timu ya Taifa ya Riadha Tanzania-3


Ron W. Davis Novemba 2018 alikuja Tanzania kwa mara ya pili.
DAR ES SALAAM, TANZANIA
Makala yaliyopita tulijikita kuangazia maisha ya awali ya mwanariadha na mwanamapinduzi katika mchezo huo Ron William Davis na namna alivyopata nafasi ya kuzuru bara la Afrika. 

Aidha katika tuliangazia namna alivyokutana na mpiganaji wa taifa la Afrika Kusini Nelson Mandela mwanzoni mwa miaka ya 1990 ambaye alitumia mchezo wa riadha kuomba radhi wanamichezo wa Afrika Kusini ambao walifungiwa kushiriki michuano tangu mwaka 1960 kutokana na vitendo vya ubaguzi wa rangi. 

Tuliona Mandela alipopaza sauti yake kwa watu wa Afrika ya Kusini walimwelewa na ikawa sababu mojawapo iliyomfanya akalie kiti cha urais wa taifa hilo mwaka 1994 ikiwa ni miaka michache baada ya kutoka jela la Rhode Island alikodumu kwa miaka 27. 

Katika makala haya tutaangazia namna alivyotua Tanzania na kuwa kocha mkuu wa timu ya riadha ya taifa. Kwa ufupi Ron Davis ndiye kocha wa kwanza kuiletea Tanzania medali pale alipomsimamia mkongwe Filbert Bayi na Suleiman Nyambui katika mashindano ya kimataifa.

MICHUANO YA JUMUIYA YA MADOLA 1978
Mwaka 1978 michuano ya Jumuiya ya Madola ilifanyika mjini Edmonton, Alberta nchini Canada. Nigeria iliamua kuwa haitashiriki michuano hiyo kwani ilikuwa imetoka kwenye michuano ya All Africa Games ambayo Ron Davis alikuwa kocha huko. 

Sababu kubwa ya Nigeria ya kutoshiriki ilikuwa wazi kabisa kwa ilikuwa imegomea kuunga mkono michuano hiyo kutokana na New Zealand kushiriki mashindano ya michezo na taifa la Afrika Kusini wakati huo ubaguzi wa rangi ulikuwa wa kiwango cha juu. 

Kitendo hicho cha Nigeria kufanya hivyo hakikuwa kigeni kwani mwaka 1972 iliongoza mgomo wa michuano ya Olimpiki ilifanyika mjini Munich nchini Ujerumani pia ilifanya hivyo katika Michuano ya Olimpiki ya mwaka 1976 iliyofanyika Montreal nchini Canada. 

Katika mahojiano na Ron Davis anasema, “Nigeria ilikuwa na msimamo wa kuunga mkono mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi ambao ulikuwa ukienea kwa kasi, na juhudi hizo zilienea duniano kote.” Ron Davis analikumbuka vema tukio hilo la michuano ya Jumuiya ya Madola kwani taifa la Canada ambao walikuwa wenyeji wa mashindano hayo walipeleka ndege yao Air Canada nchini Algeria ambayo ilitumika kuchukua wanamichezo wa Afrika ambao walikwenda kushiriki. 

Kocha huyo anasema, “Mimi, Lee Evans na John Carlos hatukupanda ndege hiyo na timu lakini tulitumia ndege ya Ujerumani kwa ufadhili wa kampuni ya Puma, kwani Carlos alikuwa akiiwakilisha Puma katika michuano ya Jumuiya ya Madola.” 

Ron Davis anasema kuwa uwepo wa Carlos uliwafaidisha kwani baada ya siku kadhaa za kuwapo mjini Herzogenaurach miongoni mwa vitongoji mahiri katika jimbo la Bavaria nchini Ujerumani yeye na Carlos walikwenda Edmonton wakati Lee aliitwa California. 

Akiwa kwenye ndege Ron Davis anasema alikuwa haamini kama anakwenda kwenye michuano hiyo akiwa kama kocha na alitabasamu tu akikumbuka miaka ya nyuma ilivyokuwa katika kufikia ndoto zake. Canada haikuwa mara yake ya kwanza lakini safari ya kutinga katika michuano hiyo kama miongoni mwa makocha wakubwa duniani ndiyo ilimfanya atabasamu ndani ya ndege. 

Wakati naandika makala haya nikakumbuka nukuu ya mwanamitindo na mwigizaji wa kike wa Marekani Christie Brinkley aliposema, “Ishirikishe dunia na tabasamu lako. Ni alama ya mahusiano mazuri (urafiki) na amani.” 

Hakika hata sasa ukimuona Ron Davis tabasamu lake bado analo hiyo ikimaanisha ndiye yule aliyetabasamu ndani ya ndege ikimaanisha ni mtu wa amani. Na amani yake ndiyo ilimfanye akutane na ujumbe kutoka Tanzania katika michuano hiyo.

HATUA MOJA MBELE
Ron Davis akihojiwa na mwandishi wa habari Jabir Johnson Novemba 2018 Mkuza, Kibaha mkoani Pwani.
Ron Davis anasema, “Siku moja nikiwa katika mazoezi ya kukimbia, yoga na kujinyoosha katika njia za Chuo Kikuu cha Alberta wakati michuano hiyo ikiendelea nilienda kwa kocha wake wakati ambaye siku hiyo alikuwa na Filbert Bayi wakifanya mazoezi.” 

Aidha Ron Davis alikuwa hajui kwa wakati huo alipokutana na kocha wa Filbert Bayi kama ingetengeneza njia. Wakati huo kocha Sulus alikuwa akimnoa Bayi. Baada ya mazungumzo ya muda Sulus alimtambuliza kwa Waziri wa Michezo na Utamaduni wa Tanzania alikuwapo Edmonton. 

Hapo ndipo walipopanga muda mzuri wa kukutana ili kubadilishana mawazo na uzoefu kuhusu mchezo wa riadha. Ron Davis anasema alishtushwa na namna mwakilishi huyo wa nchi alivyomkaribisha kutokana na kwamba alikuwa bado ni kocha wa timu ya taifa ya Nigeria ingeleta mkanganyiko lakini alisubiri nini kitakachotokea.

Unafikiri nini kilifuata baada ya Ron Davis kukutana Kocha Sulus na Waziri wa Michezo na Utamaduni katika mashindano ya Jumuiya ya Madola mwaka 1978? Tukutane juma lijalo katika mwendelezo wa makala haya.

Makala haya yametayarishwa na Jabir Johnson ambaye alipata fursa ya kuzungumza na Ron Davis  katika masuala mbalimbali ya maisha yake na medani ya riadha alipotua nchini Tanzania. Pia yalichapishwa katika Gazeti la Tanzania Daima. Kwa maoni ushauri barua pepe: jaizmela2010@gmail.com

Post a Comment

0 Comments