Thursday, March 6, 2025

Wanawake Moshi DC wazuru Gereza la Karanga; Wabubujikwa na machozi…

 

Baadhi ya wanawake wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi wakikabidhi mahitaji kwa ajili ya Wafungwa na Mahabusu wa Gereza la Karanga, Moshi katika ziara mnamo tarehe 6 Machi 2025. Msaada huo wa Hali na Mali ulipokelewa na SSP Rehema J. Okello kwa niaba ya Mkuu wa Gereza hilo. (Credit to: Jabir Johnson/ JAIZMELA)

Wanawake katika Halmashauri ya Wilaya ya Moshi wameonyesha umuhimu wa wa uungwaji mkono, usawa, na haki, baada ya kufanya ziara fupi katika Gereza la Karanga-Moshi huku wakidhihirisha huruma na utambuzi wa haki za binadamu.

Hayo yanajiri ikiwa ni siku ya Halmashauri ya Wilaya ya Moshi kuhama kutoka KDC na kuingia makao mapya Sango wilayani humo pia kuelekea kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambayo hufanyika kila mwaka tarehe 8 Machi ambapo Kitaifa yatafanyika jijini Arusha.

Akizungumza baada ya kuzuru Gereza la Karanga-Moshi Afisa Maendeleo na Mratibu wa Mikopo katika Halmashauri ya Moshi Bi. Stella Magori amesema kuenda kuwaona wafungwa na kuwasaidia kunaweza kuhamasisha jamii kuwa na mtazamo wa usawa na haki, na kwamba sio kila mtu alikosea kwa kiwango cha kuwa na adhabu ya kudumu na kwamba wafungwa wanastahili haki za kimsingi.

“Huu ni mwendelezo wa kuadhimisha siku ya wanawake duniani, tumeona ni vema kusherehekea na wafungwa na mahabusu walioko katika gereza la Karanga; wanawake wametoa michango mbalimbali ambayo imetumika kununua baadhi ya mahitaji kwa ajili ya wafungwa na mahabusu hao. Tuna la kujifunza ikiwamo kupata faraja kujimuika na kina mama wenzetu ambao hawapati nafasi ya kuwepo uraiani; kuna haja ya kwenda kuwafariji kila wakati,” amesema Bi. Stella Magori.

Akipokea msaada huo kutoka kwa wanawake wa Halmashauri ya Moshi kwa niaba ya Mkuu wa Gereza; SSP Rehema Okello wa Gereza la Karanga –Moshi amesema kitendo kilichofanywa na watumishi hao ni mfano wa kuigwa na kwamba wasisite kufanya hivyo na kuihamasisha jamii kujitolea kuwaona wafungwa na kuwatia moyo.

“Jambo mlilofanya ndugu zangu ni la kuigwa, nasi tunalipokea kwa mikono miwili kwani mnapokuja kuwaona wafungwa hawa mnawatia moyo n ahata wengine wakimaliza vifungo vyao watarudi kwenye jamii na kuwa watu wema, asanteni sana,” amesema SSP R.J Okello.

Wakizungumza kwa hisia kali wanawake walijionea hali halisi ya wafungwa katika gereza la Karanga –Moshi wamesema wamejifunza kuwa kutoa ni moyo na sio utajiri na kwamba kila mtu anastahili nafasi ya kurekebisha maisha yake, hata wale waliokosa bahati au walikosea.

Wakati mwingine, kusaidia wafungwa kunaweza kuleta mabadiliko chanya, kama vile kuongeza uelewa kuhusu haki za wafungwa, kuboresha masharti yao, na kutoa fursa za upya kwao baada ya kifungo. Hii inachangia katika kupunguza uhalifu na kusaidia mfungwa kuungana tena na jamii baada ya kutoka gerezani.







Related Posts:

0 Comments:

Post a Comment