Ukweli na Kuheshimiana ni kiini ujenzi wa jamii zetu

Ulimwenguni kwa sasa kumejaa habari potofu na upotoshaji, ni muhimu kuhakikisha kwamba ukweli na kuheshimiana vinakuwa kiini kwa ujenzi wa jamii zetu.

Mapambano dhidi ya Habari za Uongo hayapaswi kukoma

Habari za uongo, habari za uongo zinazosambazwa kwa lengo la kumdhuru mtu au jambo fulani, huifanya jamii kuwa na sintofahamu. Zinaweza kutumika kwa madhumuni ya kiitikadi, kisiasa au hata uhalifu, kama vile ulaghai mtandaoni unaolenga kuiba data ya kibinafsi.

Utandawazi na Athari zake katika Uandishi wa Habari

Katika jamii yetu ya kisasa, ambapo habari ziko kila mahali na zinaweza kupatikana kwa kila mtu, mara nyingi ni ngumu kutofautisha kati ya vyanzo vya kuaminika na habari bandia.

Uandishi wa Habari nguzo msingi mkuu kwa ujenzi wa jamii inayojitambua

JAIZMELA blog ni miongoni mwa vyanzo vya habari, zilizochakatwa kwa kuzingatia miiko ya uandishi wa habari.

Mila na Desturi ni nguzo muhimu

Mila na desturi ni nguzo muhimu sana katika utamaduni wa jamii yoyote ile; mila ni sawa na sheria zisizoandikwa. Mila ni taratibu za maisha na mwenendo zinazofuatwa na jamii fulani katika utendaji kulingana na historia na utamaduni wao. Mila zinatambulisha maadili ya jamii husika, huelezea namna jamii inavyoendesha mambo yake.

Thursday, January 30, 2025

MAMA SAMIA LEGAL AID CAMPAIGN 2025: Kushindwa kuandika Wosia kumetajwa chanzo cha migogoro ya ardhi na mirathi

Wakili Boniface Mwabukusi
Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS)

Kushindwa kuandika wosia kumetajwa kama chanzo cha migogoro ya ardhi na mirathi

Akizungumza katika uzinduzi wa wiki ya sheria mnamo Januari 29, 2025 mkoani Kilimanjaro Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS) Wakili Boniface Mwabukusi alisema Migogoro ya ardhi na mirathi ni matatizo yanayoweza kutokea kutokana na sababu mbalimbali, na mara nyingi husababishwa na mifumo ya kijamii, kiuchumi, na kisheria.

“Huduma ya Msaada wa kisheria ni ibada, ni ibada kwasababu tunashughulika na maisha ya watu ya kila siku; ni wakati wa kuifanya kwa unyenyekevu na ukamilifu wake na kuelewa kwamba hata mitume wangekuwepo leo au Yesu angekuwa Kilimanjaro sehemu ya kwanza kufika ingekuwa hapa kwenye Legal Aid,” alianza Mwabukusi

Aidha Mwabukusi alisema kuwa kutokuwa na utaratibu mzuri katika kugawa mali za marehemu, kunakosababishwa na maelezo hafifu ya wosia, au kutokuwepo kwa wosia kabisa.

“Matatizo mwakubwa na changamoto ya legal yanayogusa wananchi yapo kwenye ardhi na mirathi, na yanachangiwa na utafsiri mbaya wa sheria au watu wakorofi tu na kwenye mirathi ni kwasababu hatupendi kuandika wosia,” alisisitiza Mwabukusi.

Mwabukusi aliongeza kuwa wakati mwingine, wanajamii wanachukulia kwamba wao wanastahili sehemu fulani ya ardhi au mali ya familia, na hivyo kuleta migogoro kuhusu nani anapaswa kumiliki nini.

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu alithibitisha kuwepo kwa changamoto ya ardhi katika mkoa wake huku akitaja sababu ya ongezeko la watu na ardhi kuwa finyu.

“ Tuseme ukweli waliotanguliwa wanasema mkoa wa Kilimanjaro liko tatizo kubwa la ardhi....ni kweli....kwasababu ardhi yetu ni finyu; na ardhi hiyo ilishagawanywa kwa muda mrefu na waliokuwa nayo; na watu wanaongezeka na wazazi wanaendelea kuzaa, ili wagawane vihamba ndipo tatizo linapoanzia; ” alisema Babu.

Kwa upande wake Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbaro amesema wananchi wanapoitafuta haki wanaonyesha ustaarabu na ndio sababu ya kufanyika kwa kampeni ya utoaji wa msaada wa kisheria nchini iliyoratibiwa na Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Watu hawa wanajitokeza kwa wingi katika kampeni hii ya Mama Samia Legal Aid kwasababu wanaitafuta haki ili wakidhi kiu yao; ya kupata haki, Ukiona wananchi wanaitafuta  haki kwanza ni kuwapongeza sana kwasababu wananchi hao wamestaarabika; tunakwenda kuhakikisha Mama Samia Legal Aid inaleta Haki ambayo italiinua taifa,” alisema Dkt. Ndumbaro.

Kauli mbiu mwaka huu katika wiki na siku ya Sheria, “ Tanzania ya 2050; Nafasi ya Taasisi zinazosimamia Haki Madai katika kufikia Malengo Makuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo.”

 







Monday, January 27, 2025

Yuji ‘Gump’ Suzuki awasili Cape Town (SA) kwa mguu, baada ya siku 210

Yuji "Gump" Suzuki mnamo Januari 26, 2025 jijini Cape Town baada ya kuwasili akihitimisha safari yake ya kilometa 6,000 kutoka Nairobi, Kenya. Yuji alitumia miezi saba kutoka Juni 2024 hadi Januari 26, 2025.


“Hayo ni Maisha Yangu”; alisikika Mjapan mmoja akitamka mnamo Januari 26, 2025 katika viunga vya jiji la Cape Town nchini Afrika Kusini baada ya kuwasili akitokea Nairobi, Kenya kwa mguu.

Cha kustaajabisha ni kwamba Mjapan huyo aliyefahamika kwa jina la Yuji ‘Gump’ Suzuki aliwasili katika jiji hilo lililo umbali wa kilometa 6,400 kutoka Nairobi, Kenya akiwa na mkokoteni wa matairi mawili akiongozana na vijana wengine wawili wa Kijapan.

Mjapan Yuji mwenye umri wa miaka 34 aliwasili jijini Cape Town humo akitumia siku 210 sawa na takribani miezi saba tangu alipoianza safari yake mnamo Julai 2024, alipita nchini Tanzania, Zambia, Zimbabwe na Namibia kabla ya kuingia Afrika Kusini.

Mapema asubuhi ya Januari 26, 2025 akiwa na mkokoteni wake uliojizolea umaarufu mkubwa wa ‘Rickshaw’ wenye uzito wa kilogramu 100; Yuji aliukokota kwa furaha na kuwapongeza vijana wenzake kwa kumuunga mkono katika safari hizo za kitalii

Nisingeweza kufanya bila ninyi ndugu zangu, ninatembea kwa furaha, nimekuwa nikisafiri kwa miaka tisa sasa na nimekuwa nikiungwa mkono nanyi hivyo narudisha kwenu. Hayo ni maisha yangu,” alisema Suzuki.

Yuji aliongeza kuwa changamoto za barabarani kubwa lakini iliyokuwa ngumu zaidi ni ya kupenya Jangwa la Namibia.

Kwa mujibu wa tovuti yake; mnamo mwaka 2016-2017 Yuji Suzuki; alitembea kutoka China hadi India pia kilometa 2,500 alizunguka barani Ulaya mnamo mwaka 2017; pia kilometa 5,100 nchini Marekani kati yam waka 2022-2023.

Mkokoteni wa magurudumu mawili (Rickshaw) ulianza kutumika lini?

Rickshaw ya kwanza ilivumbuliwa nchini Ufaransa mwishoni mwa karne ya 17; kwa ajili ya mahitaji ya usafiri licha ya uwepo wa aina nyingine za vyombo vya usafiri. Miaka hiyo ya 1679 Ufaransa ilikuwa imeendelea sana katika masuala ya usafiri  aina ya “Omnibus” ambazo zilikuwa zinafanana na waendeshaji wa mikokoteni ya kuuza mvinyo katika mitaa ya jiji la Paris. Wakati huo mikokoteni hiyo ilikuwa ikisukumwa na watu wawili mmoja anakuwa mbele akivuta na mwingine nyuma akisukuma. Huyu wa mbele alikuwa akishikilia mbao fulani ikiwa ni sehemu ya kutafuta mizania na kuongoza uelekeo anaoutaka.

Wasanii wa uchoraji hawakuwa nyuma Msanii Claude Gillot alichora picha yake aliyoipa jina la “Les deux carosses” ambao ulionyesha mikokoteni hiyo miwili; mchoro huo aliuchora mnamo mwaka 1707.

Katika ardhi ya Japan, wao walivumbua kivyao mnamo mwaka 1869 ambapo kipindi cha utawala wa Tokugawa (1603-1868) kulipigwa marufuku ya matumizi ya vyombo vya usafiri vinavyotumia matairi ikiwamo mikokoteni. Wakati mikokoteni ya Rickshaw ikianza ndio kipindi ambacho Japan ilikuwa imeanza kukua katika masuala ya ufundi.

Izumi Yosuke anasalia kuwa mvumbuzi wa kwanza wa Rickshaw nchini Japan akishirikiana na Suzuki Tokujiro na Takayama Kosuke ambao wote kwa pamoja walipata wazo kutokana na namna magari ya Farasi yanavyofanya kazi, miaka michache baadaye waliyaingiza mitaani na kuwa sehemu ya maisha kisha kusambaa hadi China na kwingineko.

Credit to: Jabir Johnson/ JAIZMELA/Mashirika ya Habari/Wikipedia 

+255 693 710 200






 

Thursday, January 23, 2025

Tundu Lissu ni nani?

 

Tundu Antipas Lissu
Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA)

Tundu Lissu ni mwanasheria maarufu nchini Tanzania, na aliwahi kuwa Rais wa chama cha wanasheria Tanganyika(TLS), mwaka 2020 aligombea urais wa Tanzania kwa tiketi ya Chadema na kushindwa na mgombea wa chama tawala John Magufuli, aliyefariki dunia Machi 2021. 

Lissu aliyenusurika kifo Septemba 2017 baada ya kushambuliwa kwa risasi mjini Dodoma, ni maarufu kwa siasa za mapambano na ''ulimi mkali'' hali ambayo mara imemuweka katika mabishano makali na wanasiasa wezake hususan wa chama tawala. Amekuwa akisema alipopigwa risasi alikuwa ''nusu mfu'' 

Kuanzia mwaka 2010 Lissu alikuwa mbunge wa Singida Mashariki na alijipatia umaarufu kwa michango yake bungeni hususan ya kuikosoa serikali ya Rais Jakaya Kikwete na baadaye Hayati Rais John Pombe Magufuli.

Lissu ni msomi wa kiwango cha shahada ya umahiri aliyoipata nchini Uingereza katika Chuo Kikuu cha Warwick kati ya mwaka 1995 na1996. Kabla ya hapo alipata shahada ya kwanza ya sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam alikohitimu mwaka 1994. 

Maisha yake yamekuwa zaidi katika harakati za kutetea haki za binadamu na kutoa msaada wa kisheria kwa watu wenye mahitaji lakini wana uwezo mdogo wa kifedha. Aliwahi pia kuwa mwenyekiti wa chama wanasheria za Mazingira Tanzania (LIT) katika miaka ya 1990.

Sunday, January 5, 2025

China Communication Construction Company kuanza ujenzi barabara ya Ndungu-Mkomazi

 

Wakala wa barabara Nchini (TANROADS) wametakiwa kuhakikisha wanatoa kipaumbele kwa wazawa kwenye miradi ya ujenzi barabara na kuwawezesha vijana kupata ajira kwa lengo la kuinua uchumi wa wananchi .

Waziri wa ujenzi Abdalla Ulega ametoa agizo hilo alipokuwa Wilayani Same mkoani Kilimanjaro katika hafla ya kumkabidhi mkandarasi CHINA COMMUNICATION CONSTRUCTION COMPANY (CCCC) mradi wa ujenzi wa barabara ya Ndungu -Mkomazi yenye urefu wa kilomita 36 itakayo tengenezwa kwa kiwango Cha lami ikiwa ni utekelezaji wa mpango wa serikali kuhakikisha Uwepo wa Maendeleo na ufanisi katika sekta ya usafiri na usafirishaji.

Ulega amesema ujenzi wa barabara hiyo utaondoa kero ya usafiri pia kuimarisha na kuchochea Kasi ya uchumi ,kilimo, biashara na utalii hususani kwa wananchi wote wa wilaya ya Same, Kanda ya kaskazini na Pwani.

"Serikali imetoa fedha zaidi ya bilioni 59 kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii ya Ndungu -Mkomazi itakayowakomboa wananchi kiuchumi hivyo vijana changamkieni fursa za ajira zitakazotokana na ujenzi wa barabara hii,zalisheni kwa wingi Mpunga,Tanga wizi na ndizi ili kukuza mtandao wa biashara Kati ya Same ,Mikoa ya Tanga na Pwani" amesema Waziri Ulega.

Kutokana na umuhimu mkubwa wa ujenzi wa barabara hiyo utakao rahisisha huduma ya usafiri na usafirishaji amesisitiza vijana wa maeneo yanayopitiwa na mradi wa ujenzi kuchangamkia fursa za ajira zitokanazo na mradi huo.

Awali Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro amesema ujenzi wa barabara hiyo inayopita kwenye idadi kubwa ya wananchi Wilayani humo utarahisisha Maisha na kuibua fursa nyingi za kiuchumi .

Barabara ya Ndungu- Mkomazi ni Moja ya barabara muhimu hapa nchini hususani katika shughuli za Maendeleo zinazochochea uchumi wa nchi kupitia kilimo,utalii na biashara na kwa kuliona hilo serikali imeshakamilisha malipo ya awali takribani bilioni 5.8 kwa mkandarasi ili kuanza kazi rasmi ya ujenzi wa kilomita 36 kwa kiwango Cha lami.

Credit to: Elizabeth Mkumbo; Freelancer/JAIZMELA